2013-09-25 08:06:17

Kanisa Katoliki Burkinafaso, halitatuma wajumbe katika Seneti


Ouagadougou (Agenzia Fides) –
Kanisa Katoliki nchini Burkina Faso limesema halitatuma wajumbe kuliwakilisha kwenye bunge Senate la nchi hiyo. Kwa tamko hilo, Baraza la Maaskofu Katoliki la Burkina Faso limekatalia mbali pendekezo la sheria ya nchi hiyo iliyopitishwa mwezi Mei ambayo inawania kuyapa nafasi kadaa makundi ya kidini kutuma wajumbe kwenye bunge la nchi hiyo. Wabunge hao wangechaguliwa na viongozi wa kidini ili kuweza kuwasilisha maslahi ya dini zao.

Hata hivyo, Baraza la Maaskofu Katoliki nchini humo linasema kwamba Kanisa Katoliki litaendelea kusimama na ukweli wa mafundisho yake, kamwe haliwezi kwenda kinyume na msimamo wake kwa kuwatuma wawakilishi kwenye uongozi wa kisiasa, na kwamba maaskofu hao wataendelea kutekeleza wajibu wao wa kutoa mwelekeo na msimamo wa Kanisa hata kuhusiano na mambo ya uongozi, bila kujihusisha kisiasa kwa kuwapeleka wawakilishi maalum.

Lengo la Kanisa ni kuendeleza mshikamano na amani kwenye jamii ya wananchi wote na hata kama kuna lazima, kusimama na upinzani ikiwa utakuwa unasimamia haki na mafao ya wananchi wote.

Kuanzishwa kwa Bunge la Senate nchini Burkina Faso kumeshuhudia maandamano ya kupinga hatua hiyo, huku watu wengi wakihofia kwamba Senate hiyo itatumika kama chambo na rais wa nchi hiyo, Bw. Blaise Compaoré ili kuendeleza mafao yake mwenyewe na hasa katika kugombea tena kiti cha urais kwenye uchaguzi mkuu ujao wa 2015.

Mwezi Julai Maaskofu wa nchi hiyo walipinga vikali kuanzishwa kwa Bunge la Senate nchini humo, wakihofia kwamba jambo hili huenda likaathiri amani nchini Burkina faso.











All the contents on this site are copyrighted ©.