2013-09-10 08:01:10

Mwombeni Mama Maria, Malkia wa Amani, kwa ajili ya amani dunian


Mama Kanisa anamheshimu mama Bikira Maria kama Malkia wa Amani. Naye baba Mtakatifu Francisko, alipotoa mwito wa sala, mafungo na mkesha kwa ajili ya kuomba amani kwa ajili ya Syri, Mashariki ya Kati na dunia nzima, aliuomba ulimwengu mzima umwangalie Mama Maria kama mwombezi wa binadamu mbele yake Mwenyezi Mungu.

Hivyo siku ya Jumamosi wakati wa kesha ya sala kwa ajili ya amani, Mama Bikira Maria alichukua nafasi ya kipekee sana. Mbali na kusali Rozari Takatifu kwa pamoja, kulikuwepo pia sanamu ya Bikira Maria inayoenziwa kama sanamu ya zamani zaidi katika historia ya Kanisa.

Sanamu hiyo ijulikanayo kama Salus Populi Romani inahifadhiwa kwenye madhabahu moja ndani ya Kanisa kuu la Maria Maggiore lililoko mjini Roma tangu mwaka 1611. Kuna tamaduni inayosadiki kwamba sanamu hiyo ilichorwa na Mtakatifu Luka. Hata hivyo inaaminika kuwa ni mchoro wa karne ya 12, ambao unamwonyesha Maria akiwaelekeza binadamu njia ya kufuata, Yesu Kristo.

Miujiza mingi imesemekana kutendeka kutokana na sanamu hiyo kama ule wa karne ya Kumi na sita, pale mji wa Roma ulipokumbwa na ugonjwa wa tauni, naye Baba Mtakatifu Pio V akaichukua sanamu hiyo kwenye maandamao ya sala hadi Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro. Inasemekana kuwa kabla ya kulifikia Kanisa hilo, wote waliokuwa kwenye maandamano hayo waliona kile walichokiita Malaika Mikaeli kwenye mlima Adriani. Kutokana na muujiza huo Baba Mtakatifu alitabiri kuwa ile ilikuwa ishara ya tauni kumalizika, na kweli, baada ya muda mfupi, iliisha kabisa. Kilima hicho hata leo kinajulikana kama ngome ya Malaika Mtakatifu Mikaeli.

Mchoro huo pia ulitumika kwenye maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani iliyofanyika Tor Vergata Agosti, 2000 ambapo Baba Mtakatifu Yohanne Paolo II aliwakabithi vijana wote mikononi mwa Mama Bikira Maria.

Baba Mtakatifu Francisko amewahi kusali mbele ya mchoro huo mara kadhaa tangu kuchaguliwa kwake kama khalifa wa Mtakatifu Petro, kama vile wakati wa kuanza mwezi wa rozari, Mei 2013, kabla ya kuelekea, na baada ya kurudi kutoka Brazil kwenye maadhimisho ya Siku 28 ya Vijana duniani mwaka huu. Hii ni ishara ya mapendo makubwa aliyo nayo Papa kwa Mama wa Mkombozi Yesu Kristo. Naye anawaalika watu wote wa mapenzi mema kumtazama Mama huyu aliye Malkia wa Amani awezaye kuwaonyesha njia ya amani kwa ajili ya Syria, Mashariki ya katin a dunia nzima.








All the contents on this site are copyrighted ©.