2013-09-07 11:23:19

Barua ya Papa Francisko kwa Rais Putin


Uchumi wa kimataifa utaendelea kukua kama tu utafuata mfumo wenye kuyaheshimu na kuyajali maisha na hadhi ya binadamu wote, kuanzia aliye mkubwa zaidi hata yule angalipo bado tumboni mwa mama yake, sio tu kwa wananchi wanchi ishirini zenye uchumi mkubwa zaidi duniani, lakini hata kwa kila mwananadunia, hata wale walio vijijini na wenye kusukumizwa pembezoni mwa jamii.

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko kwenye barua aliyomuandikia Rais Vladimir Putin wa Russia, ambaye pia ni rais wa mkutano mkuu wa nchi ishirini zilizo na uchumi mkubwa zaidi duniani, (G20), zilizofanya mkutano wao wa mwaka, mjini Petersburg, Urusi mwishoni mwa wiki (tarehe 05 na 06/06/2013) .

Kwenye barua yake, Baba Mtakatifu Francisko alimkumbushia Rais Vladmir wajibu alio nao kwa kushehenewa cheo cha urais wa mataifa hayo ishirini yenye uchumi mkubwa zaidi duniani, huku akisema kwamba nchi ya Russia imehudhuria mikutano yote tangu mwanzo wa G20 na kwamba rais huyo ameamua kuhakikisha kwamba biashara ya kimataifa itaendeshwa kistaarabu ili kuweza kukabiliana na changamoto zinazoletwa na myumbo wa kiuchumi duniani.

Papa alisema kwamba ni wazi kwamba migogoro na kinzani ya kivita inayoshuhudiwa sehemu nyingi za dunia ni matokeo ya ubinafsi na kutotaka kuendeleza biashara na mahusiano yenye kuchangia maendeleo endelevu na mafao ya wengi. Ni kukataa makusudi kutafuta na kufuatia amani kwa kuendeleza mahusiano ya kibiashara yenye kuyaheshimu maisha ya wengine; hivyo kusababisha mahangaiko, njaa, magonjwa na hata vifo kwa watu wengi sana sehemu mbalimbali za dunia.

Anasema Baba Mtakatifu kwamba bila amani haiwezekani kuwa na maendeleo ya kweli ya kiuchumi, na kwamba utumiaji wa mabavu kamwe haujengi amani inayohitajika sana kwenye maendeleo ya kina.

Japo viongozi hao wa mataifa ishirini yenye nguvu ya kiuchumi hawakuwa wanalenga kuzungumzia maswala ya usalama duniani kwenye mkutano wao wa mwaka, Baba Mtakatifu aliwaalika kulimulikia swala la Mashariki ya Kati na hasa Syria huku akisema alisikitika kwamba tangu mwanzo wa migogoro ya Syria kumekuwa na kutokubaliana kwa ajili ya kupendelea upande fulani fulani, hivyo kuongeza ugumu wa kutafuta suluhu ya amani nchini humo.

Baba Mtakatifu alimwalika kila mmoja wa viongozi hao kusaidia kutafuta suluhisho la amani na wala sio kwa njia ya utumiaji wa silaha, bali kwa majadiliano ambayo ndiyo yanayopendelewa na jumuiya ya kimataifa, huku akiongezea kwamba serikali zote zinao wajibu wa kimaadili kuwasaidia wenye kukumbwa na mahangaiko na mateso, hata nje ya mipaka ya nchi zao wenyewe.











All the contents on this site are copyrighted ©.