2013-09-05 11:32:21

Katekesi ya Papa ya Jumatano: Vijana tumaini la kanisa na dunia


Vijana ni tumaini la Kanisa na dunia nzima na hivyo inawapasa kushiriki kikamilifu kwenye shughuli zote za kikanisa na kijamii kwa ajili ya mafao ya watu wote. Ndiyo changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko siku ya Jumatano hapa mjini Vatikan. Baba Mtakatifu Francisco pia amemshukuru mwenyezi Mungu na wote waliofanikisha safari yake nchini Brazil hivi karibuni ambapo aliweza kujumuika na mamilioni ya vijana kutoka sehemu mbalimbali za dunia kwenye maadhimisho ya 28 ya siku ya vijana duniani.

Papa ameirejea safari yake ya kichungaji nchini Brazil wakati wa Katekesi yake, Jumatano, tarehe 4 Septemba 2013 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, uliokuwa umefurika kwa umati mkubwa wa waamini, mahujaji na watu wenye mapenzi mema.

Amesema japo ni zaidi ya mwezi tangu akamilishe safari yake hiyo, lakini ameona umuhimu wa kukumbushia yale yaliyotokea wakati wa maadhimisho hayo, akisema kwamba kwake yeye aliye mzaliwa wa bara la Marekani ilikuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Amemshukuru pia Bibi Yetu wa Aparecida kwa ufanisi huo akisema kwamba Bikira Maria daima amekuwa kiini cha imani Brazil. Amesema yeye binafsi, pamoja na ndugu zake maaskofu walishirikiana kwa karibu kabisa na Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto wa Kumi na sita kwa kazi ya kichungaji barani humo ambapo wanaishi wakristo wakatoliki wengi zaidi duniani.

Kwa mara nyingine tena Baba Mtakatifu amewashukuru viongozi wa kidini na wale wa kiserikali, mashirika ya kikatoliki na yale ya kiekumeni, makampuni na watu binafsi, maparokia na miji na vijiji waliochangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha safari yake. Ni safari ilyofanyika ndani ya mwaka wa imani ambamo pia Mama Kanisa anaadhimisha miaka hamsini tangu Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatikani.

Amewataja kuwa watu wa nguvu – WaBrazili – kwa namna walivyoonyesha mambo maku matatu – Ukarimu, Sherehe na Umissionari.

Watu wa Brazil walionyesha Ukarimu wao kwa Papa kwa namna walivompokea kwa moyo mkuu, moyo mkunjufu na mapendo adili; Amesema papa kuwa siku ya vijana duniani ni sherehe kwa wote kwani wakati vijana waliojaa furaha wanapofika kwenye mji fulani basi na wenyeji pia hufurahi na kusheherekea pamoja nao. Ndivyo ilivyotokea hata na Brazil. Ila Brazil kulikuwa na sherehe kubwa zaidi, sherehe ya imani, wakti kwa pamoja vijana na wasio vijana waliungana kumsifu na kumtukuza Mungu, na kukesha huku wakilisikiliza neno lake Mungu na kuyatafakari matendo makuu ya Mungu. Amesema Papa kuwa bila mapendo ya kiMungu hakuwezi kuwa na karamu ya kikweli kati ya binadamu.

Mwishoni baba Mtakatifu amesema kuwa moyo wa kimissionari ulijidhihirisha wazi kwenye sherehe za maadhimisho ya Siku ya Vijana Brazil sanjari na maneno ya Kristo mwenyewe – E nendeni mkayafanye mataifa yote kuwa wanafunzi wangu. Baada ya kulisikiliza neno la Mungu vijana walitumwa kulihubiri kote duniani.

Baba Mtakatifa aliwachangamotisha vijana waliokuwa wanamsikiliza kwenye wuwanja wa kanisa Kuu la Mtakatifu Petro kuwa wafuasi wa kristo akisema kwamba kwenye vijana kuna pia tumaini. Vijana nao walimshabikia Baba Mtakatifu Francisko kwa vifijo na kushangilia kwa furaha pale alipowaomba kufungua milango ya mioyo yao na kumwalika kristo na kuwa tumaini la Kanisa na dunia nzima.











All the contents on this site are copyrighted ©.