Mshikamano na Wakristo wanaodhulumiwa nchini Misri
Baraza la Maaskofu Katoliki Uswiss linapenda kuonesha mshikamano wake wa dhati kwa
Wakristo wanaoishi Misri na Mashariki ya Kati, wakati huu wanapokabiliana na hali
ngumu ya maisha kutokana na vita, vurugu na kinzani za kijamii zinazoendelea kusababisha
maafa makubwa katika maeneo haya.
Maaskofu wa Uswiss wanasema, Wakristo nchini
Misri wanaishi katika mazingira hatarishi na kwamba, Kanisa nchini Uswiss linaungana
na waamini wanaodhulumiwa na kunyanyasika kutoka na imani yao kwa Kristo na Kanisa
lake, ili waweze kupata ujasiri wa kusonga mbele pasi na kukata tamaa. Jumamosi na
Jumapili iliyopita, Baraza la Maaskofu Katoliki Uswiss limetolea Ibada za Misa Takatifu
kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwaombea wananchi wanaoishi Misri na Mashariki ya Kati
hususan nchini Syria, ili waweze kupata amani na utulivu kwa njia ya majadiliano ya
kweli.
Kanisa Katoliki nchini Uswiss limetolea Ibada ya Misa kwa ajili ya
wote wanaoendelea kudhulumiwa na kukosewa haki, ili mioyo ya watu wengi zaidi iweze
kumwongokea Mwenyezi Mungu ambaye ni chemchemi ya amani na upendo. Vita inasababisha
maafa makubwa kwa watu na mali zao. Ni jambo la kusikitisha kuona kwamba, nyumba za
Ibada, Miundo mbinu ya elimu, afya na maendeleo ya Jamii inaharibiwa kwa chuki zisizo
na msingi.
Maaskofu wa Uswiss wanasema kwamba, inatia moyo kuona kwamba, waamini
wengi wa dini ya Kiislam wanaguswa na kusikitishwa na vitendo vya dhuluma na nyanyaso
dhidi ya Wakristo. Hizi ni dalili njema kwamba, bado kuna uwezekano wa kuishi kwa
amani na utulivu, kila mtu akiheshimu na kuthamini dini na imani ya jirani zake.
Maaskofu
wanaendelea kuungana na watu wenye mapenzi mema kuitaka Serikali ya Misri kutafuta
ufumbuzi wa machafuko ya kisiasa nchini humo kwa njia ya kidiplomasia na majadiliano
kwa kuheshimu na kuthamini uhuru wa kidini. Baraza la Maaskofu Katoliki Uswiss linapanga
kupeleka msaada wa hali na mali kwa njia ya Shirika la Misaada la Kanisa Katoliki,
Caritas.