2013-08-26 10:13:35

Machafuko ya kisiasa nchini Misri, wakristo wanaendelea kunyanyasika zaidi!


Askofu Kyrillos William Samaan wa Jimbo Katoliki la Assiut katika mahojiano na Shirika la Kipapa la Misaada kwa ajili ya Makanisa hitaji anasema kwamba, machafuko ya kisiasa nchini Misri yaliyowaka moto hapo tarehe 3 Julai 2013 kwa kumwondoa madarakani Rais Mohamed Mursi kwa njia za kijeshi, kumepelekea Wakristo wengi kudhulumiwa.

Baadhi ya Waislam wenye msimamo mkali wanadhani kwamba, hizi ni njama za Wakristo kutaka kutawala Misri. Mwelekeo huu potofu wa kudumaa kwa demokrasia ya kweli, utawala wa sheria na uhuru wa kuabudu, kumepelekea Wakristo kuanza kunyanyaswa kana kwamba, wao ndio chanzo cha machafuko ya kisiasa nchini Misri.

Inasikitisha kuona kwamba, kuna baadhi ya Waamini wanatumia machafuko ya kisiasa nchini Misri kwa kuchoma nyumba za ibada na miundo mbinu ya huduma msingi za kijamii jambo ambalo ni hatari sana kwa maisha na ustawi wa wananchi wa Misri kwa siku za baadaye. Kutokana na mwelekeo wa sasa, Wakristo ndio wanaoendelea kulipia gharama ya machafuko ya kisiasa nchini Misri.

Kuna haja kwa Waislam na Wakristo kujenga utamaduni wa majadiliano ya kidini, ili kwa pamoja waweze kusimama kidete kulinda na kutetea zawadi ya uhai, mafao ya wengi, demokrasia na utawala wa sheria unaoheshimu uhuru wa kuabudu na kwamba, raia wote wa Misri wana haki sawa na wala hakuna raia wa daraja la pili kutokana na imani yake.

Kinzani na madhulumu yanayojitokeza miongoni mwa wananchi wa Misri yanahitaji upatanisho na msamaha wa kweli unaopata chimbuko lake kutoka katika undani wa moyo wa mwamini mwenyewe. Wananchi wote wa Misri washirikiane kwa pamoja ili kufanya mabadiliko ya dhati yatakayozingatia mafao ya wengi nchini Misri pamoja na kutetea haki msingi za binadamu.








All the contents on this site are copyrighted ©.