2013-08-24 09:27:07

Imani ni nguvu msingi katika ujenzi wa amani!


Vitendo vya kigaidi venye asili ya uchochezi wa kidini, kinzani za kisiasa, kijamii na kikabila ni kati ya mambo ambayo yameendelea kuchangia kuporomoka kwa misingi ya haki na amani sehemu mbali mbali za dunia. Hakuna sababu za msingi zinazoweza kuhalalisha vitendo vya kigaidi na uvunjifu wa amani na kwamba, mwanadamu kimsingi ni mtu mwenye imani na wala hakuna utamaduni usiojengeka katika msingi wa imani.

Uhuru wa kidini ni msingi wa haki nyingine zote za mwanadamu, unaoonesha uhusiano kati ya mwanadamu na Muumba wake na kati ya wanadamu wenyewe. Ni wajibu wa Serikali husika kuhakikisha kwamba, inatoa haki sawa kwa raia wake katika masuala ya uhuru wa kidini, kama sehemu ya mchakato wa kulinda na kudumisha mafao ya wengi. Demokrasia ya kweli inawajibu wa kuthamini uhuru wa kidini, uhuru wa kuabudu na ule wa mwamini kutoa mawazo na maoni yake.

Haya ni baadhi ya mawazo msingi yaliyotolewa na Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini wakati alipokuwa anashiriki kwenye mkutano wa urafiki miongoni mwa watu wa Mataifa mjini Rimini, nchini Italia. Uhuru wa kidini unagusa dhamiri ya mtu, mahali patakatifu panapomwezesha mtu kutambua jema la kufuata na baya la kuepuka. Uhuru wa kidini ni sehemu ya vinasaba vya ukweli na wala si jambo la shuruti kutoka nje.

Imani ni jambo shirikishi linalowajumuisha watu wanaoamua kufuata: Ibada, Imani na Mafundisho pamoja na kujenga uhusiano wa dhati na Mwenyezi Mungu, jambo la hali ya juu kabisa ambalo mwanadamu anaweza kulitenda bila kizuizi kutoka nje. Dini inaonesha uhusiano wa mwanadamu na Mwenyezi Mungu; kiumbe na Muumba wake. Madhehebu mara nyingi yanaonesha ili hali ya binadamu kutaka kutawala nguvu za Kimungu kwa ajili ya mafao yake binadamu.

Kardinali Tauran anasema kuna haja kwa Serikali na dini mbali mbali kushirikiana kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wengi na kwamba, waamini wa dini mbali mbali duniani wanalo jukumu la kuchangia maendeleo ya nchi zao. Waamini ni rasilimali watu inayoweza kutumika kwa ajili ya mafao ya wengi. Kumbe, kuna haja ya kulinda na kudumisha tunu msingi za maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili. Waamini wapewe nafasi ya kushiriki katika Ibada; wawe na uhuru wa kushirikiana na watu wengine imani yao na kwamba, kwa pamoja waamini wana dhamana ya kulinda na kudumisha amani.

Kardinali Tauran anabainisha kwamba, imani ni nguvu msingi katika ujenzi wa amani. Kwani hapa utu na heshima ya binadamu inapewa kipaumbele cha kwanza; daima waamini wakichangamotishwa kusimama kidete kutafuta mafao ya wengi; wakielimishana katika ukweli na uwazi; maadili na utu wema ili kujenga Jamii inayosimikwa katika udugu, upendo na mshikamano wa kweli.

Tofauti za kiimani kamwe zisiwe ni chanzo cha vurugu na kinzani za kijamii, bali kikolezo cha mshikamano wa dhati. Waamini wa dini mbali mbali wanapaswa kuwa ni mfano na ushuhuda wa misingi ya maadili na utu wema. Dini ikiondolewa katika maisha ya mwanadamu, hapo patakuwa ni patashika nguo kuchanika!







All the contents on this site are copyrighted ©.