Rais Kikwete na changamoto za elimu nchini Tanzania
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete ameyapatia ufumbuzi
matatizo makubwa na ya muda mrefu ambayo yamekuwa yanawakabili wahadhiri na wanataaluma
wa Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki vya Umma nchini.
Katika kikao kilichofanyika
Ikulu, Dar Es Salaam Jumatano, Agosti 21, 2013 kwa muda wa saa sita kati ya Rais na
Viongozi wa Muungano wa Wanataaluma wa Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki vya Umma
nchini wakiongozwa na Mwenyekiti wao Prof. Remmy Assey kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine,
na kuhudhuriwa pia na Makamu wa Rais Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal na Katibu
Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Y. Sefue, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya
Mrisho Kikwete aliamua na kuelekeza ifuatavyo:
(1) Serikali, kupitia Wizara
ya Fedha, ihakikishe kuwa Bajeti ya Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki vya Umma ambayo
imekuwa inapungua mwaka hadi mwaka inarejeshwa kwenye viwango vya zamani mapema iwezekanavyo,
na kwamba bajeti hiyo isiwe inapungua mwaka hadi mwaka kama ilivyo sasa.
(2)
Nyongeza ya fedha hizo itumike kuboresha mazingira na miundombinu ya kufundishia
katika Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki vya Umma. Shughuli hiyo ianze kwa kufanyika
tathmini ya kujua vipaumbele, na kuandaa mpango mahsusi wa utekelezaji.
(3)
Madai ya wanataaluma yatokanayo na stahili zao, na ambayo yamehakikiwa yalipwe kwa
awamu na kazi ya uhakiki wa madeni mengine iendelee.
(4) Serikali kupitia
Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, ishirikiane na Viongozi wa Vyuo hivyo
kupitia upya Muundo wa Utumishi (Scheme of Service) kwa ajili ya wanataaluma kwa lengo
la kuuboresha kwa kuzingatia mahitaji maalum ya wanataaluma.
(5) Vyuo
Vikuu vya Umma virejeshewe uhuru wa kuajiri wanataaluma moja kwa moja bila ya shughuli
hiyo kufanywa na Sekretarieti ya Ajira Serikalini.
(6) Ofisi ya Rais, Menejimenti
ya Utumishi wa Umma ikutane na Viongozi wa Muungano wa Wanataaluma haraka iwezekanavyo
ili kupata ufumbuzi wa matatizo ya upandishaji vyeo wanataaluma na nyongeza za mishahara
za kila mwaka.
(7) Utaratibu wa Mikopo ya Ujenzi wa Nyumba kwa ajili ya Watumishi
wa Serikali ulioanzishwa na Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania, uhusishe pia Wanataaluma wa Vyuo Vikuu. Aidha, Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu
Vishiriki vyenye ardhi ya kujenga nyumba za kuishi wanataaluma vijadiliane na Mifuko
ya Hifadhi ya Jamii yenye wanachama kwenye vyuo hivyo ili kuona uwezekano wa Mifuko
hiyo kujenga nyumba za kuishi za wanataaluma kwenye maeneo hayo.
(8) Mifuko
ya Hifadhi ya Jamii na Mdhibiti wa Mifuko hiyo washirikiane haraka na Vyuo Vikuu na
Vyuo Vikuu Vishiriki vya Umma pamoja na Serikali ili kulipatia ufumbuzi tatizo la
uwasilishaji wa michango ya pensheni ya wanataaluma.
Rais na viongozi wa wanataaluma
hao wamekubaliana kukutana tena baada ya miezi mitatu kupokea taaarifa ya utekelezaji
na kufanya maamuzi kuhusu maeneo mengine yanayoendelea kuchambuliwa kwa kushirikiana
kati ya Serikali, Uongozi wa Vyuo na Uongozi wa Muungano wa Wanataaluma.
Viongozi
wa Muungano wa Wanataaluma wa Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki vya Umma nchini walimshukuru
Rais kwa hatua hizi na maamuzi yake katika kushughulikia matatizo yao ya siku nyingi
na kuahidi kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuyapatia ufumbuzi matatizo yaliyobaki.