2013-08-22 08:41:24

Ukosefu wa fursa za ajira unawatumbukiza wengi katika umaskini wa kipato!


Mtandao wa Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Nchini Uingereza, CSAN, limepokea taarifa ya Serikali ya Uingereza kuhusu kupungua kwa ukosefu wa fursa za ajira nchini humo, lakini umeiomba Serikali kuendelea kujifunga kibwebwe ili kuhakikisha kwamba, inajipanga barabara kukabiliana na tatizo la ukosefu wa fursa za ajira nchini Uingereza kama sehemu ya mchakato wa kupambana na umaskini wa hali na kipato.

Katika kipindi cha kuanzia mwezi Aprili 2013 hadi Mwezi Juni 2013, takwimu za kitaifa zinaonesha kwamba, watu 4,000 walikosa fursa za ajira nchini Uingereza. Hali hii ina madhara makubwa kwa wafanyakazi pamoja na familia zao wanaoendelea kukabiliana na hali ngumu ya maisha kwani kuna baadhi ya familia zinashindwa kupata mahitaji yake msingi kutokana na ukata wa maisha ambao umechangiwa kwa kiasi kikubwa na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Zaidi ya watu millioni tano wanapokea mshahara ambao hauwezi kukidhi mahitaji msingi ya familia, hali ambayo inaendelea kuwatumbukiza watoto wengi nchini Uingereza katika hali ya umaskini. Hii ni kashfa ya umaskini inayowaandama wafanyakazi wanaoendelea kupokea mshahara usiokidhi mahitaji msingi ya wafanyakazi.

Mtandao wa Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki nchini Uingereza unaendelea kuihamasisha Serikali kuhakikisha kwamba, inatoa mishahara ya haki na mafao msingi kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya wafanyakazi, kama sehemu ya mchakato unaopania kuleta mabadiliko katika mfumo wa ajira unaozingatia haki.

Hii ni changamoto iliyotolewa na Askofu mkuu Vincent Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza, hivi karibuni alipokuwa anazungumza na wajumbe wa Mtandao wa Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki nchini Uingereza.

Alisema, balaa la umaskini linaendelea kushika kasi ya ajabu nchini Uingereza, kiasi kwamba, wafanyakazi wengi wanajikuta wanapokea mishahara ambayo haikidhi gharama za maisha, kiasi cha kuwafanya kuwa ni tegemezi kwa Mabenki ya chakula kwa ajili ya mikopo ya chakula kila mwezi. Hii ni changamoto kwa Serikali, Sekta binafsi na Jamii kwa ujumla na kwa wote ambao wanapaswa kutoa maamuzi ya kina kwa ajili ya wafanyakazi na familia zao.








All the contents on this site are copyrighted ©.