2013-08-22 11:00:57

Siku ya Makatekista Kitaifa Brazil


Makatekista ni kati ya wadau wakuu wa azma ya Uinjilishaji ndani ya Kanisa kwani jukumu lao kubwa ni kuwaandaa Wakatekumeni ili waweze kupokea vyema Sakramenti za Kanisa. Makatekista wengi wamekuwa ni mfano na mwanga kwa Jumuiya inayowazunguka.

Kanisa linaendelea kuwashukuru Makatekista kwa mchango wao katika maisha na utume wa Kanisa. Hili ni kundi ambalo linahitaji kupatiwa majiundo ya kina na endelevu ili liweze kutekeleza dhamana na wajibu wake ndani ya Kanisa. Lakini, wanapaswa kulindwa na kuheshimiwa, kwani mfanyakazi mwaminifu katika shamba la Bwana anastahili kupata ujira wake.

Makatekista wanaendelea kuchangamotishwa na Mama Kanisa kuhakikisha kwamba, wanatoa ushuhuda wa imani tendaji kwa njia ya maisha na matendo yao adili, kwa kuwajali wote bila ubaguzi. Ni mwaliko wa kumwilisha Injili na Mafundisho ya Mababa wa Kanisa, ili kutoa Katekesi safi na kina kwa watu wao; wakiwaongoza kwa moyo wa Sala na Ibada. Kama sehemu ya viongozi wa Kanisa wanapaswa kutekeleza wajibu wao kwa ujasiri na bidii, ili kuchangia utakatifu wa maisha ya Familia ya Mungu inayowajibika.

Hivi ndivyo alivyoandika Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika Waraka wake wa kichungaji, Africae Munus.

Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil, Jumapili tarehe 25 Agosti 2013 linaadhimisha Siku ya Makatekista Kitaifa. Uwepo wao ni mchango makini ulioliwezesha Kanisa Katoliki nchini Brazil kuwafikia watu waliokuwa pembezoni mwa Jamii. Makatekista wamechangia kwa kiasi kikubwa azma ya Uinjilishaji nchini Brazil. Siku ya Makatekista Kitaifa nchini Brazil ni sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita.

Maadhimisho haya yanafanyika wakati Kanisa Katoliki Brazil bado lina kumbu kumbu hai ya yale yaliyojiri katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013, Brazil ilipofunikwa kwa uwepo wa mamillioni ya vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia pamoja ushuhuda wa imani na matumaini uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko.

Maaskofu Katoliki Brazil wanasema, Katekesi za kina zilizoendeshwa na Maaskofu wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani yameacha chapa ya kudumu. Wengi wamejifunza kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko ambaye kwa wakati huu amekuwa kweli ni kielelezo cha Katekista mkuu anayefundisha kwa mifano ya ushuhuda wa maisha na maneno yanayoacha chapa ya kudumu katika maisha ya watu.

Baba Mtakatifu amewagusa wengi kiasi cha kufufua furaha ya ndani, imani na matumaini ya kusonga mbele bila ya kukata tamaa. Huu ndio mchango wa Katekesi mang'amuzi ya maisha; Katekesi inayofumbatwa na Neno la Mungu na Kumwilishwa katika maisha ya Jumuiya ya waamini.







All the contents on this site are copyrighted ©.