2013-08-21 11:10:10

Zingatieni ukweli, uaminifu na umakini katika taarifa zenu!


Kanisa la Kikoptik la Kiorthodox nchini Misri katika ujumbe wake kwa vyombo vya habari lina laani vitendo vyote vinavyofanywa kinyume cha maisha ya kiroho, kimaadili na kiutu na kwamba wananchi wote wanapaswa kusimama kidete kupinga vitendo hivi vinavyohatarisha maisha, ustawi na maendeleo ya wananchi wa Misri katika ujumla wao.

Viongozi wa Kanisa hili wanaendelea kuwaombea wote waliofariki dunia kutokana na machafuko ili wapate pumziko la milele; majeruhi waweze kupona haraka na kurudi tena katika shughuli zao za kila siku, huku wakipania kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani na utulivu. Viongozi hawa wanavitaka pia vyombo vya habari vya kimataifa kuhakikisha kwamba, vinatekeleza wajibu wao barabara kwa kuzingatia misingi ya: ukweli, uaminifu na umakini.

Wanawaomba wananchi wa Misri kujikita katika mchakato wa majadiliano ya kina na upatanisho wa kweli ili kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa. Kanisa la Kikoptik linalaani mauaji ya askari kuwa ni kitendo cha kinyama kwani hawa walikuwa wanatekeleza dhamana na wajibu wao kwa taifa. Viongozi hao wanasema, wasingependa kuona mataifa ya nje ya kiingilia mambo ya ndani ya Misri kwa hali inaweza kuwa ni mbaya zaidi.

Kama viongozi wa Kanisa wanatumaini huruma na ulinzi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, atakayewaimarisha na kuwawezesha kujenga tena nchi yao upya katika misingi ya haki, amani, utulivu na demokrasia ya kweli.







All the contents on this site are copyrighted ©.