2013-08-21 08:46:51

Tarehe rasmi ya kuwatangaza Yohane XXIII na Yohane Paulo II kuwa watakatifu kujulikana rasmi hapo tarehe 30 Septemba 2013


Baba Mtakatifu Francisko hapo tarehe 30 Septemba 2013 anatarajiwa kutangaza tarehe rasmi kwa siku ambayo amechaguwa ili kuwatangaza Wenyeheri Yohane wa XXIII na Yohane Paulo II kuwa kwenye orodha ya watakatifu wa Kanisa. Hayo yamebainishwa na Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu wakati wa mahojiano maalum na Radio Vatican.

Baba Mtakatifu siku hiyo, atakuwa na mkutano wa kawaida na Makardinali kutoka sehemu mbali mbali za dunia ili kujadili ombi la kuwatangaza waamini walionesha mifano bora ya kuigwa katika maisha na utume wao ndani ya Kanisa. Ni Baba Mtakatifu peke yake ambaye kwa sasa anafahamu tarehe hiyo maalum, kinyume cha baadhi ya taarifa zilizokuwa zimeenea kwenye vyombo mbali mbali vya habari kwamba, Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili angeweza kutangazwa mwaka huu.

Kardinali Angelo Amato anasema, Mwenyeheri Yohane wa XXIII alikuwa Nabii na Muasisi wa Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Mwenyeheri Yohane Paulo II akafafanua na kumwilisha Mafundisho ya Mtaguso wa Pili wa Vatican katika maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro. Viongozi hawa wawili ni miamba wa utamaduni na utakatifu wa maisha ya Kikristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.