Mwaka wa Imani na Ibada maalum kwa Bikira Maria: 12-13 Oktoba 2013
Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto wa XVI, Kanisa katika Mwezi Oktoba litaadhimisha Mwaka wa Imani
kwa kutoa kipaumbele cha pekee kwa Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa.
Kuanzia
tarehe 12 hadi 13 Oktoba, kutakuwa na Maadhimisho maalum ambayo yatamshirikisha Baba
Mtakatifu Francisko pamoja na vyama vyote vya kitume vinavyochota tasaufi yake kutoka
kwa Bikira Maria. Tukio hili limeandaliwa na Baraza la Kipapa kwa ajili ya Uinjilishaji
mpya. Hii ni sehemu ya Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili
wa Vatican na Miaka 10 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipochapisha kwa mara
ya kwanza Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki.
Tukio hili ni sehemu ya kumbu
kumbu ya Bikira Maria alipowatokea watoto watatu wa Fatima yaani: Francisko, Yacinta
na Lucia, hapo tarehe 13 Oktoba 1917. Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Sanamu
ya Bikira Maria wa Fatima italetwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro
mjini Vatican, ili waamini na watu wenye mapenzi mema waweze kutoa heshima yao kwa
Bikira Maria wa Fatima.
Ratiba elekezi inaonesha kwamba, hapo tarehe 12 Oktoba
2013 kuanzia Saa 2:00 asubuhi kwa saa za Ulaya, waamini watafanya hija kuzunguka kaburi
la Mtakatifu Petro, watapata nafasi ya Kuabudu Ekaristi Takatifu na Sakramenti ya
Upatanisho kutoka kwenye Makanisa yanayolizunguka Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini
Vatican.
Jioni saa 11:00. Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kupokea Maandamano
ya Sanamu ya Bikira Maria wa Fatima kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro
na hapo Baba Mtakatifu atatoa Katekesi ya kina kuhusu Ibada kwa Bikira Maria. Sanamu
hii itapelekwa kwenye Madhabahu ya Bikira Maria ya "Divino Amore" hapa Roma kwa ajili
ya kusali Rozari Takatifu, itakayowaunganisha waamini kutoka kwenye Madhabahu ya Bikira
Maria yaliyotawanyika sehemu mbali mbali za dunia. Saa 4:00 Usiku, kutafanyika kesha
la Sala kwa Bikira Maria.
Jumapili tarehe 13 Oktoba 2013, Sanamu ya Bikira
Maria wa Fatima itarudishwa kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro. Saa 4:
30 Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu. Askofu mkuu
Rino Fisichella anasema, Ibada hii ni utashi ulioneshwa kwa namna ya pekee na Baba
Mtakatifu Francisko kwa ajili ya heshima na ibada kwa Bikira Maria Mama wa Mungu na
Kanisa.
Itakumbukwa kwamba, Baba Mtakatifu Francisko ana ibada ya pekee kwa
Bikira Maria, ambaye hivi karibuni alijiweka chini ya ulinzi na usimamizi katika maisha
na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.