2013-08-20 07:08:55

Umuhimu wa kukuza na kudumisha majadiliano ya kidini kwa njia ya elimu


Kituo cha Kimataifa cha Majadiliano ya Kidini na Kitamaduni (Kaiciid) kilichoanzishwa kwa ushirikiano wa Falme za Kiarabu, Hispania, Australia na Vatican ikiwa ni nchi mwanachama mtazamaji na mwanzilishi, bado kinaendeleza majadiliano ya kidini na kitamaduni katika nchi mbali mbali. RealAudioMP3

Hapo tarehe 26 Agosti 2013, kauli mbiu itakayoongoza Warsha ya siku moja ni “taswira ya mwingine”. Warsha ambayo itafanyika Addis Ababa, Ethiopia kwa ajili ya Bara la Afrika.

Mada hii inalenga kukuza na kuendeleza elimu na majiundo ya majadiliano ya kidini na kiakili miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali Barani Afrika. Wajumbe 130 kutoka katika sekta ya dini na elimu wanatarajiwa kushiriki. Mada hii inatarajiwa kufanyiwa kazi kwa kipindi cha miaka mitatu. Itakumbukwa kwamba, Mwaka 2013 ni elimu, Mwaka 2014 utajadili kuhusu njia za mawasiliano ya kijamii na mwaka 2015 wajumbe watapembua kwa kina na mapana ulimwengu wa mtandao.

Mada hii itaendelea kujadiliwa Barani Asia na Amerika na kuhitimishwa kwa mkutano wa kimataifa utakaofanyika hapo tarehe 18 hadi 19 Novemba 2013 huko Vienna, Austria.

Itakumbukwa kwamba, Kituo cha Kimataifa cha Majadiliano ya Kidini na Kitamaduni kilianzishwa rasmi kunako tarehe 26 Novemba 2012 kwa lengo la kuhamasisha, kurahisisha, kukuza na kujenga majadiliano ya kidini miongoni mwa wafuasi wa dini mbali mbali duniani, ili kujenga dunia inayosimikwa katika utamaduni wa ushirikiano, heshima katika tofauti za kiimani, haki na amani.

Mfalme Abdullah Bin Abdulaziz, Mfalme wa Falme za Kiarabu, alipokutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, hapo tarehe 6 Novemba 2007, aliomshirikisha nia ya kuanzisha Kituo cha Kimataifa kwa ajili ya majadiliano ya kidini na kitamaduni. Wakati wa uzinduzi wa kituo hiki, Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini alimwakilisha Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika shughuli hii.

Alisema katika hotuba yake kwamba, Kituo hiki cha Kimataifa, ilikuwa ni fursa nyeti ya ujenzi wa jukwaa la majadiliano katika medani mbali mbali za maisha ya waamini. Uhuru wa kuabudu ni mada muhimu sana kwa waamini wote. Kituo hiki kinatambulika na Umoja wa Mataifa kama Jukwaa na nafasi ya majadiliano kwa kutoa fursa muhimu kwa watu wenye uzoefu na mang’amuzi makubwa kuweza kushirikisha matunda ya majadiliano ya kidini miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali.

Akizungumzia kuhusu Kituo hiki cha Kimataifa, Padre Federico Lombardi, msemaji mkuu wa Vatican alibainisha kwamba, Vatican inaweza kuchangia kwa kiasi kikubwa uzoefu na mang’amuzi yake katika majadiliano ya kidini.








All the contents on this site are copyrighted ©.