2013-08-20 08:23:55

Cheche za Neno la Mungu: Jengeni moyo wa ukarimu!


Ukoo wangu ni dhaifu...

Somo la Kwanza : (Waamuzi 6:12 - 24)

Mungu anamtokea Gideoni, Mwamuzi (Judge) wa kwanza baada ya kifo cha Joshua ili afanye kazi yake ya kuwaongoza kwa muda Waisraeli. katika vita. Visingizio vya unyonge wa Gideoni kuwa ni kutoka kabila dhaifu na wa mwisho katika familia yake, vilitolewa hata na Musa (sijui kuongea), Yeremia (mimi ni mdogo) na Isaya (nina midomo michafu). Kazi ya Mungu haitegemei akili zetu, nguvu zetu, ufundi wetu - bali unyoofu na ukubali wetu. Roho wa Mungu atatujalia cha kusema na cha kutenda kama zawadi iliyoshuka siku ya Pentekoste kwa mitume.

Mungu anamchukua kamanda wa mgambo, askari asiye mzoefu, mtu mshamba wa kijijini. Mungu anajua mapungufu yote ya Gideoni lakini bado anamchagua na kuwekeza wito wote huu katika chombo cha udongo. Mungu anamjenga kisaikolojia Gideoni kuwa atakuwa naye daima katika vita na uongozi wake. Sadaka anayotoa Gideoni, Mungu anaishiriki kwa kutuma moto uiteketeze.

Somo la Injili : (Mt 19:23 - 24)

Ni rahisi kwa ngamia kupenya tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa mbinguni. Mitume wanashangaa sana. kristu anawashusha wasi wasi wao na kuwaambia kuwa hii kwa Mungu inawezekana (Mt 19:26).

Masomo yetu ya leo Agosti 20, 2013 yanatuambia :

1. Mungu wetu akitupa kazi yake huwa hatuachi peke yetu - "nipo pamoja nanyi hadi ukamilifu wa dahari.."(Mt 28:20). Mungu hatuachi peke yetu katika mapambano ya ndoa zetu. Mungu daima anawasindikiza wana ndoa na kuwafanyia miujiza pale tunapomwalika Kristu kama walivyofanya wale wa harusi ya Kana (Yoh 2:1 - 11). Shida tuipatayo katika ndoa zetu ni pale ambapo tunapowaalika wazazi na mashangazi zetu tu wakati tunapotofautiana. Kristu akiwa kati yetu tutaweza kusikia sauti yake ndogo - msamehe mwenzako.. !


2. Kujipunguza, kujiachia na kujibandua katika mali zetu ni kupata mara mia hapa duniani na uzima wa milele mbinguni. Hii haimaanishi kwamba kuwa tajiri ni kitu kibaya au ni dhambi, ila kwamba Kristu anataka tujijenge katika moyo wa ukarimu. Mtume Paulo aliwasifu sana Kanisa la Wafilipi kwa utajiri wao wenye kusheheni ukarimu, kwa kusaidia Kanisa la Yerusalem (Wafilipi 4:14-20). Wema daima huwa hauozi. Tujisikie faraja na fahari tunapowasaidia wengine wenye shida.

Tusali kwa kuomba roho ya ukarimu kwa familia zetu. Pia tuombee kazi zetu ambazo wakati mwingine zinazidi kimo na uwezo wetu.


Tafakari hii inaletwa kwako kwa njia ya mtandao na
Padre Beno Michale Kikudo,
Jimbo kuu la Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.