Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba Jaji Joseph Warioba amesema Tume yake haishawishi
wananchi wakubali mapendekezo yaliyomo katika Rasimu ya Katiba waliyoiandaa kama inavyodaiwa
na baadhi ya watu lakini hulazimika kutoa ufafanuzi pale inapohitajika.
Jaji
Warioba alitoa ufafanuzi huo mjini Morogoro Jumamosi, Agosti 17, 2013, wakati akijibu
swali la mmoja wa Wajumbe wa Baraza la Katiba la Manispaa ya Morogoro aliyeomba ufafanuzi
wa Tume kuhusu kauli za baadhi ya wanasiasa kuwa Tume yake inashawishi Wajumbe wa
Mabaraza kukubali rasimu ya Katiba.
“Mna haki ya kuuliza na kupata ufafanuzi
na sisi kama Tume tuna wajibu wa kutoa ufafanuzi kwa yale mnayouliza katika mikutano
… huo sio ushawishi ni ufafanuzi,” alisema Mwenyekiti huyo akijibu swali la mjumbe
huyo Bw. Dotto Rangimoto.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, Wajumbe wa Tume wanaoendesha
mikutano ya Mabaraza ya Katiba nchini huulizwa maswali mbalimbali na wananchi wanaohudhuria
mikutano hiyo wakitaka ufafanuzi wa mambo mbalimbali yaliyomo katika rasimu ya katiba.
“Tusipojibu
tutakuwa watu wa ajabu sana,” alifafanua Mwenyekiti huyo katika mkutano uliofanyika
katika ukumbi wa Chuo cha Ualimu Kigurunyembe mjini Morogoro.
Ufafanuzi wa
Itikadi ya Ujamaa ndani ya Katiba
Katika mkutano huo, Jaji Warioba pia alifafanua
kuhusu misingi ya ujamaa na kujitegemea katika rasimu ya katiba iliyoandaliwa na Tume
yake. Jaji Warioba amesema Tume yake imependekeza katika rasimu ya katiba uwepo wa
Dira na Malengo ya Taifa ambayo yatapaswa kutekelezwa na serikali ya chama chochote
kitakachokuwa madarakani.
“Ujamaa ni itikadi lakini kujitegemea sio itikadi
… na baada ya kuanza kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa, tulikubaliana kuwa vyama
vitakuwa na itikadi tofauti,” alisema Mwenyekiti huyo na kufafanua kuwa mapendekezo
ya Tume yake yanalenga kutekeleza malengo ya taifa na sio itikadi ya chama chochote
kitakachokuwa madarakani.
Ufafanuzi wa Jaji Warioba ulitokana na swali la Mjumbe
wa Baraza hilo Bw. Andrew Tarimo aliyetaka kujua itikadi ya inayopendekezwa na Tume
baada ya ile ya ujamaa na kujitegemea kuondolewa katika rasimu iliyoandaliwa na Tume
na kuzinduliwa Juni 3 mwaka huu.
“Rasimu imeweka dira na malengo ambayo yatasimamiwa
na chama chochote bila kujali itikadi ya chama hicho,” alisema. Baraza la katiba la
Manispaa ya Morogoro limemaliza mkutano wake wa siku tatu yaani Jumamosi, Agosti 17,
2013) uliohudhuriwa na wananchi 155 kutoka kata 29 za Manispaa hiyo. Jumatatu, Agosti
19, 2013 Baraza la Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro nalo linatarajiwa kuanza mkutano
wake wa siku tatu kwa ajili ya kujadili na kutoa maoni kuhusu Rasimu ya Katiba.