2013-08-19 08:01:59

Familia na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi, sayansi na teknolojia


Familia zetu zinaishi katika ulimwengu, na hatuwezi kujitenga na ulimwengu huu wakati bado tunaishi. RealAudioMP3
Tunapoendelea kutafakari mada yetu ya familia na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi, sayansi na teknolojia katika mwaka huu wa imani, inafaa pia kutafakari ni jinsi gani familia zetu zinaweza kufaidika na maendeleo haya lakini vile vile ni jinsi gani familia zetu zinaweza kupoteza mwelekeo.
Hawali ya yote inatupasa sisi wanafamilia wote tumshukuru Mungu kwa maendeleo ya Sayansi na Teknolojia. Haya ni mapendo makubwa ya Mungu yanayoiangazia akili ya mwanadamu kutafuta njia mbadala ya kurahisisha maisha yetu ya kila siku.
Kwa mfano nikijaribu kutazama miaka ishirini iliyopita kabla simu za mikononi au mambo ya intaneti hayajaingia katika jamii zetu nyingi, mawasiliano yalikuwa magumu sana. Kama mtu amepata tatizo kwa mfano la msiba au natataka kuwasiliana na familia yake, na yeye anaishi mbali na nyumbani kwake ilikuwa inachukua hata majuma mawili kupata taarifa au kupeleka salamu. Leo hii Sayansi na Teknolojia imetuweka karibu zaidi kwa kuweza kupata mawasiliano mara moja.
Mara nyingi sisi binadamu pale tunapofanikiwa katika maisha kwa namna yoyote kuna kishawishi cha majivuno au kulewa mafanikio na kujiona kuwa mafanikio yote yametokana na jitihadi zetu binafsi na kumweka Mungu pembeni. Majivuno katika mafanikio yoyote ni hatari ya kusahu mchango wa Mungu katika mafanikio yetu. Kinyume cha majivuno ni unyenyekevu.
Katika unyenyekevu tunaalikwa kutambua uwepo wa Mungu katika maisha yetu na kuelewa sisi tunabaki kuwa binadamu ambao bila yeye hatuwezi lolote. Tukilikumbuka hilo, tutakumbuka kutoa shukrani kwa Mungu kwa zawadi mbalimbali anazotujalia katika maisha.
Tukumbuke kuwa ni Mungu anayetujalia hekima ya kuweza kutumia maendeleo haya ya vizuri, kwa faida ya maisha yetu na faida ndugu zetu tunao ishi nao. Hekima hii ya Mungu imefunuliwa kwetu kupitia Maandiko Matakatifu na Mama Kanisa akiongozwa na Roho Mtakatifu amepewa jukumu rasmi la kuendelea kufundisha ufunuo huo kwa vizazi hata vizazi “hata ukamilifu wa dahari”(Mt. 28:20) .
Bila hekima kutoka kwa Mungu, tutatumia maendeleo ya Sayansi na Teknolojia kwa ajili kujiangamiza pamoja na familia zetu. Tukuchukulie katika mazingira yetu ya kawaida mfano wa matumizi ya simu, mitandao, luninga nk. Vyombo hivyo ni vizuri sana kwaajili ya maendeo ya mwanadamu, lakini vyombo hivyo visipotumika kwa busara yaani kwa matumizi sahihi na kwa wakati sahihi huku tukizingatia maadili yetu ya Kikristo vinaweza kusambaratisha maisha ya familia na taifa la Mungu kwa ujumla.
Kwa mfano, katika nyakati za sasa tupo tayari kutumia masaa mawili kwenye intaneti au kutazama luninga au kuzungumza kwenye simu lakini tunaweza kukosa hata dakika kumi kwa siku za kufanya sala za familia au kusoma neno la Mungu. Vile vile badala ya kutumia vyombo hivi katika kueneza habari njema tunaweza kuvitumia kwaajili ya kueneza habari mbaya zenye kutengeneza chuki na uadui katika familia zetu na jamii nzima kwa ujumla.
Maendeleo yoyote katika maisha yetu sisi binadamu yanakuwa ni hatarishi pale yanapochukua nafasi ya Mungu na kuyafanya miungu yetu. Matokeo yake badala ya vyombo hivi kutusaidia kutujenga, vinasaidia kutuharibu.
Siku za nyuma katika maisha ya familia, kulikuwa na nafasi ya baba na mama kukaa pamoja na kuwaeleza watoto jinsi ya kuishi maisha bora na pale kunapotokea kasoro kurekebishana. Lakini katika wakati huu wa sasa nafasi kama hizo zinazidi kupotea tukifikiria kuwa, familia kukaa pamoja na kufanya mazungumzo kuhusu maisha yamepitwa na wakati.
Wahenga walisema, “mali bila daftari huisha bila habari”, maisha ya familia pia bila kufanyiwa tathmini tumetoka wapi, tupo wapi na tunakwenda wapi, yanaweza kutupelekea kupoteza tunu nzuri za maisha ya kifamilia. Tujaribu kujiuliza kila mmoja wetu kwa nafasi zetu, ni wangapi kati yetu tunakuwa na muda wa kukaa na familia zetu na kufanya tathmini ya mwelekeo wa familia kwaajili ya kuboresha maisha yetu?
Mambo hayo tunaweza kuyaona ni madogo lakini yasipo pewa kipaombele madhara yake ni makubwa kwa siku za usoni. Sisi bibadamu mara nyingi tunapopatwa na shida ndipo tunapoweza kumkumbuka Mungu na kumwomba atusaidie. Mungu wetu tunayemuabudu sio Mungu wa wakati wa shida tu bali ni Mungu aliyopo wakati wote.
Hivyo basi, tumshirikishe mafanikio yetu katika Nyanja zote za maisha kwa kumshukuru, na pia tumshirikishe yale tuliyoshindwa kuyatimiza kutokana na mapungufu yetu ya kibinadamu kwa kuomba neema zake kusudi tujaliwe nguvu ya kuweza kuanza upya.
Siku hii ya leo tumshukuru Mungu kwa karama mbalimbali alizotujalia kwa lengo la kutaka kuifanya dunia hii sehemu nzuri ya kuishi na tuombe hekima ya kuweza kutumia zawadi ya maendeleo ya Sayansi na Teknolojia kwa sifa na utukufu wa Mungu.
Kutoka Studio za Radio Vatican ni mimi Padre Titus Nkane, OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.