2013-08-17 10:41:14

Wananchi wa Mloganzila watoa kipaumbele cha kwanza kwa mafao ya wengi!


Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amesema atasimamia suala la fidia kwa wakazi 91 waliobakia kulipwa katika eneo la Mloganzila nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam ili liweze kuisha mwezi ujao na malipo yaandaliwe mara baada ya taratibu zote kukamilika.

Alikuwa akizungumza katika mkutano wa dhadhura, Ijumaa, Agosti 16, 2013) uliosababishwa na wakazi wa Mloganzila na vitongoji vyake ambao wanadai fidia ili wapishe mradi mkubwa wa ujenzi wa Chuo Kikuu cha Tiba na Hospitali unaotarajiwa kuanza hivi karibuni.

Kwa mujibu wa ratiba yake, Waziri Mkuu alikuwa ameenda Mloganzila kukagua eneo la mradi huo na kupata maelezo kwa watendaji kuhusu kusuasua kwa mradi huo.

Alisema kwa utaratibu wa kawaida wa makusanyo ya Serikali, suala hilo linaweza kufanyika mwezi Oktoba na malipo yao yataanza kupatikana Novemba mwaka huu lakini kwa vile amesikiliza hoja zao, atafuatilia na kuhakikisha malipo hayo yanawahi kidogo.

“Kwa tarehe ya leo, hata nifanye nini hatuwezi kuwahi kukamilisha malipo haya mwisho wa mwezi huu (Agosti). Na hii ni kwa mujibu wa taratibu za kifedha. Nitafuatilia ili mpewe kipaumbele katika makusanyo ya mwezi ujao,” alisema.

Kwa mujibu wa tathmini iliyofanyika mwaka 2008 na kurudiwa mwaka 2011, wakazi hao wanatakiwa kulipwa sh. milioni 980.6/-. Wakazi wengine 2,533 walikwishafanyiwa tathmini na kulipwa fidia ya sh. bilioni 9.55/-.

Katika mkutano huo baadhi ya wakazi waliopewa nafasi kuelezea kero zao, walilalamikia kuhusu viwango vidogo vya fidia walizopewa, kutolipwa fidia kwa baadhi ya wakazi ambao walikwisha kufanyiwa tathmini, na malipo yaliyotolewa kutolingana na ukubwa wa maeneo yao waliyokuwa wakiishi.

Akijibu hoja hizo, Waziri Mkuu Pinda alisema chanzo cha mgogoro huo ni baadhi ya wakazi kudai walipwe fidia ya ardhi wakati eneo hilo si lao bali lilikuwa ni mali ya kiwanda cha kusindika nyama cha Tanganyika Packers lililokuwa likitumika kunenepesha mifugo kabla haijapelekwa kiwandani.

“Tatizo hapa ni matumizi mabaya ya ardhi. Waliopewa eneo hawakuliendeleza, waliliacha wazi kwa muda mrefu na tena hawakulizungushia uzio. Hali hii ilileta vishawishi kwa watu kuanza kujipenyeza kushoto na kulia,” alisema.

Alisema anakubaliana na madai ya wakazi 91 kutolipwa fidia zao lakini wale 2,533 lazima wakubali kwamba tayari walikwishalipwa fidia ya maendelezo ya eneo walilokuwa wakiishi.

Akizungumzia kuhusu mradi wa chuo na hospitali ya Mloganzila, Waziri Mkuu Pinda aliitaja mipango ya haraka ya kuendeleza eneo hilo kuwa ni kutengeneza barabara ya kilometa 12 itakayounganisha eneo kuu la chuo hicho. ”Huduma nyingine ambazo ni lazima zipatikane haraka ni maji na umeme. Ili mradi uende kwa kasi, ni lazima hizi huduma zipatikane mapema,” alisema.

Aliwapongeza wakazi hao kwa uamuzi wao wa kukubali kupisha mradi wa ujenzi wa chuo hicho uendelee kwa vile wanatambua kwamba una maslahi kwa Taifa. ”Nimefurahi kusikia kwamba mnataka mradi huu uendelee kwa vile mnatambua umuhimu wake,” aliongeza.

Mara baada ya mkutano huo, Waziri Mkuu alipokea maelezo kuhusu maandalizi ya ujenzi wa mradi huo kutoka kwa watendaji wa taasisi za Serikali kama TANROADS, TANESCO, Wizara ya Maji, Wizara ya Elimu na Kamishna wa Ardhi.

Katika mkutano huo, Waziri Mkuu alifuatana na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid. Wengine ni Wakuu wa mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.








All the contents on this site are copyrighted ©.