2013-08-17 08:21:47

Pasi na fursa za ajira, utu na heshima ya binadamu iko mashakani!


Baba Mtakatifu Francisko hivi karibuni alikazia suala la kazi na thamani ya utu na heshima ya binadamu. Kazi ni muhimu sana katika kudumisha hadhi ya mwanadamu kwani inampa mtu fursa ya kuweza kukidhi maisha binafsi na familia yake na hatimaye, kuchangia katika mchakato wa maendeleo endelevu ya jamii anamoishi na kufanya kazi. RealAudioMP3

Kwa bahati mbaya mamilioni ya vijana wa kizazi kipya yanakosa kuthaminiwa na kupewa heshima inayostahili kwa kila mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa mwenyezi Mungu, kutokana na ukosefu wa fursa za ajira,, utendaji wa kazi katika mazingira duni, dhuluma na unyanyasaji wa wafanyakazi katika maeneo ya kazi.

Hii ni changamoto anayoigusia pia Askofu Stephen Blaire wa jimbo la Stockton katika siku ya wafanyakazi inayoadhimishwa nchini Marekani hapo tarehe 2 Septemba, 2013. Siku ya wafanyakazi ni wakati muafaka wa nchi yoyote ile kuangalia na kuona jinsi inavyowajali wafanyakazi wake, anasema Askofu Blare ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya haki na Maendeleo ya Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani.


Kila mwanadamu anayo haki msingi ya kuheshimiwa sio kwa sababu ya cheo alichonacho katika jamii, bali kwa sababu ameumbwa kwa sura na mfano wake Mwenyezi Mungu, kama anavyosema Mtakatifu Paulo kwenye Nyaraka zake akisema: mjitahidi katika kuoneshana wema. Tamaduni mamboleo ya watu kushindana inawalazimisha kung’ang’ania ushindi kwa mafao binafsi, lakini Mtakatifu Paulo anatoa changamoto ya kuheshimiana, kujenga kidugu na kuthaminiana kiutu.

Hata wakati uchumi wa nchi ya Marekani unaonekana kuimarika, Askofu Blaire anasema bado hali ya maisha ya watu wengi hasa maskini na wale wa kipato cha chini yanaonekana kuwa magumu zaidi kwani watu wengi bado hawana fursa za ajira na kwamba, gharama ya maisha imepanda wakati hali ya maisha inazidi kuporomoka.

Zaidi ya watu milioni nne hawana kazi kwa zaidi ya miezi sita sasa, bila hata kuhesabu mamilioni ya watu ambao tayari wamekata tamaa ya kupata kazi, kwani kwa kila nafasi ya kazi inayopatikana, huwa kuna angalau watu watano wanayoipigania. Pengo hili la kikazi limesababisha kushuka kwa mishahara nchini humo ambapo zaidi ya watu milioni 46, milioni kumi na sita kati yao wakiwa ni watoto, wanakumbwa na umaskini.

Askofu Blaire anasema Kwamba, kuna uhusiano kati ya fursa za ajira, mishahara na umaskini, kwani uchumi wa nchi hiyo hautengenezi nafasi za kutosha za ajira ili kuwawezesha wafanyakazi kuyamudu maisha yao, na kwamba, ili kupunguza pengo linalojionyesha kati ya watu wa kipato cha juu na maskini, kuna umuhimu wa kutengeneza ajira muafaka, zenye kutoa mishahara ya kuwawezesha wafanyakazi na familia zao kuishi maisha yenye heshima na hadhi ya binadamu.

Katika Waraka wake wa kichungaji Caritas in Veritate, Upendo katika Ukweli, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, anatoa maneno ya kinabii anaposema kwamba, tofauti kubwa za mishahara zinaongeza tofauti hata kwenye jamii, jambo ambalo lina madhara makubwa. Hadhi ya mwanadamu na matakwa ya haki, hasa kwa vijana wa kizazi kipya, uamuzi wa kukuza miundo ya kiuchumi yenye maadili yatakayochangia kupunguza tofauti hizi, na kuhakikisha usalama wa kazi kwa kila mtu ni mambo msingi.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita anasema kwamba, miundo mbinu inayoleta tofauti za kijamii sio tu inaathiri mahusiano ya kijamii, bali pia huyumbisha hata uchumi wenyewe, ambao unachangia sehemu kubwa ya maendeleo ya jamii husika.

Askofu Stephen Blaire anasema inasikitisha kuona kwamba maneno ya waraka wa Gaudium et Spes (no. 63), uliotokana na Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, miaka 50 iliyopita bado yanaonekana hata leo kwamba: wakati watu wengine hawapati hata mahitaji msingi ya kimaisha, kuna wengine kwenye jamii hiyo hiyo wanaoponda maisha kana kwamba hawaoni yanayowazunguka. Kwa namna hii, Jamii inawezaje kusema kwamba, watu wanaheshimiana na kujaliana kidugu?

Ni dhahiri kwamba, watu wengi wanatamani kuishi kwenye jamii inayosimikwa kwenye misingi ya haki na usawa, huku kila mtu akipata fursa ya kuboresha maisha yake. Tofauti zinazoonekana zinaweza kupunguzwa, lakini kunahitajika ujasiri katika kuendeleza mfumo unaozipunguza tofauti hizi na kujenga zaidi usawa kwenye nyanja za ajira na kipato. Hata uwezo wa makampuni kugawana na wafanyakazi wake sehemu ya faida inayotokana na michango yao makini.

Pia kunahitajika mikakati maalumu kwa ajili ya kuwasaidia wasio na kazi na wale wasio na hata uwezo wa kuweza kufanya kazi. Kama familia ya Mungu, Kanisa, jamii, mashirika ya kijamii na yale ya kibinafsi na hata serikali ina wajibu katika kukuza heshima na hadhi ya wafanyakazi.

Vyama vya wafanyakazi vimekuwa mstari wa mbele kusimama kidete kutetea haki za wafanyakazi na kama njia muafaka ya wafanyakazi hao kujishughulisha kwa karibu zaidi kwenye maamuzi yanayowahusu yanayofanywa na vitengo vyao vya kazi. Mafundisho Jamii ya Kanisa Katoliki yamekuwa mstari wa mbele kwa kusisitiza haki na uhuru wa wafanyakazi katika kushiriki kwenye vyama vinavyotetea masilahi yao.

Kuongezeka kwa tofauti kwenye mishahara kunaashiria tatizo moja, wafanyikazi kutojishughulisha na vyama vinavyoshughulikia maslahi yao. Ni kweli kwamba vyama hivi kama vyama vyovyote vile, sio vikamilifu, lakini ni muhimu kwavyo kuhakikisha havipotezi lengo muhimu la kuhakikisha mfanyakazi anapata mishahara na faida zingine zote anazostahili ili kumwezesha kuishi kwa heshima.


Vyama hivi pia vinapaswa kuhakikisha kiwango cha chini cha mishahara kinapandishwa, mazingira ya kazi ni salama kwa wafanyakazi na afya zao. Kanisa nalo liko tayari kusaidiana na vyama hivyo ili kuhakikisha wafanyakazi wanaheshimiwa na kupewa haki zao msingi.

Mashirika binafsi huchangia sana uchumi wa nchi na mafao ya wengi. Hata hivyo, ni kinyume na maadili kutafuta faida kwa kuwanyanyasa wafanyakazi na kutoheshimu hadhi yao. Mashirika haya hayana budi kujenga mshikamano unaowaheshimu wafanyakazi na wote walio pembezoni mwa jamii, kwani uchumi wowote ule ni kwa ajili ya watu, na kwamba, hatari kubwa huingia pale imani, utu na maadili yanapokosekana kwenye shughuli za kibiashara.

Ni changamoto kwa Kanisa Katoliki nchini Marekani kuunga mkono mashirika yanayolinda na kutetea maisha na heshima ya mwanadamu; kulipa mishahara ya haki na kutetea haki msingi za wafanyakazi. Pia Kanisa linapaswa kutetea utengenezaji wa sheria zitakazowasaidia wahamiaji nchini humo kujitokeza wazi na kuweza kufanya kazi kihalali, kwani ukosefu wa sheria kama hizo unawafanya wahamiaji wengi kunyanyaswa, na wengine kuendeleza shughuli kwa uficho. Ni vizuri pia kuwasaidia kupata uraia wale wanaostahili, ili waweze nao kufaidika kihalali.


Ni vizuri kuwaheshimu wafanyakazi wahamiaji kwani hata Marekani ilijengwa na wahamiaji waliokimbia mateso, unyanyasaji na umaskini kwingineko, na kuelekea Marekani ili kujipatia fursa ya kutumia vipaji vyao kwa uhuru zaidi kwa mafao yao wenyewe na ya familia zao. Kuwakaribisha wageni, wakimbizi, wahamiaji, na wale wote wanaosukumizwa pembezoni mwa jamii kama watoto wa Mungu ni wajibu wa kila mkriso.

Lakini, ni muhimu zaidi kudhibiti hali zote za: kisiasa, kijamii na hata kiuchumi zinazosababisha watu kuyakimbia makazi na nchi zao. Mshikamano wa kidugu unamaanisha kuwaheshimu wafanyakazi mahali popote pale walipo.

Askofu Stephen Blaire anasema uchungu umezidi kwa maskini na maskini wapya wanaotokana na mwendelezo wa mfumo wa uchumi unaokuza tofauti kwenye jamii na akawasihi watu wote wenye mapenzi mema kusimama kidete ili kutetea haki ya kazi, mishahara ya kutosha na kuilinda hadhi ya mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mwenyezi Mungu.

Lengo la maadhimisho ya siku ya wafanyakazi mwaka huu nchini Marekani, iwe ni kuitikia mwito unaotolewa kila inapohitimishwa Ibada ya Misa Takatifu kwenda kuitangaza Injili ya matumaini na mshikamano kwa wale walioathirika kwa myumbo wa uchumi kimataifa.

Imehaririwa na Sr. Bridgita Samba Mwawasi,
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.