2013-08-17 08:31:16

Mikakati ya Wasalesiani wa Don Bosco katika Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 200 tangu kuzaliwa kwa Mtakatifu Don Bosco


Mheshimiwa Padre Pascual Chavez, Mkuu wa Shirika la Wasalesiani wa Don Bosco anasema, wakati huu wanapojiandaa kwa Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 200 tangu alipozaliwa Don Bosco ni mwaliko na changamoto kwa Wanashirika kuchota katika mang’amuzi ya maisha ya kiroho ili kuweza kufanya hija ya utakatifu wa maisha mintarafu karama, maisha na utume wa Shirika la Wadon Bosco. RealAudioMP3

Kwa mwaka 2014 wanaalikwa kwa namna ya pekee kujichotea utajiri wa maisha ya kiroho unaobubujika kutoka kwa historia na maisha ya Mtakatifu Don Bosco.

Tasaufi ya maisha yao kama Shirika, inafumbatwa katika upendo wa shughuli za kichungaji unaowawajibisha kutafuta na kuendeleza utukufu wa Mungu na kwa ajili ya wokovu wa binadamu. Wanatambua kwamba, kama Wanashirika, wanawajibishwa na upendo wa Kristo kama Maandiko Matakatifu yasemavyo “Caritas Christi urget nos” Upendo wa Kisalesiani unajikita zaidi katika shughuli na mikakati ya kichungaji kwa ajili ya wokovu wa roho za watu; hali inayojionesha kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika sekta ya elimu na majiundo ya vijana.

Wasalesiani hawana budi kujitosa kimasomaso kutumia nguvu na karama zao kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya vijana wanaowahudumia. Lengo anasema Padre Pascual Chaves ni kuwajengea vijana uwezo wa kuwa ni: raia wema, Wakristo hodari na raia wa maisha ya uzima wa milele.

Ni wajibu kwa Wanashirika kutambua mambo msingi kwa maisha ya Mtakatifu Don Bosco, shughuli na mikakati yake ya kichungaji na mbinu aliyotumia katika kuwapatia vijana elimu, lakini zaidi, Wanashirika wajitaabishe kufahamu undani wa maisha yake ya kiroho uliomwezesha kujenga na kuwa na mazoea mazuri na Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yake. Ufahamu huu, ujikite zaidi katika tafiti makini na upembuzi yakinifu ili hatimaye, kugundua kiini cha tasaufi ya Mtakatifu Don Bosco, inayoweza kufahamika kwa wazazi wa vijana wanaowahudumia.

Kwa mwaka 2014, anasema Padre Pascual Chavez, Wasalesiani watafanya tafakari kuhusu mang’amuzi ya tasaufi ya Mtakatifu Bosco; upendo na ari ya shughuli za kichungaji na kwamba, tasaufi hii ni dira kwa miito yote. Huu ni mwelekeo wa maisha ya Mtakatifu Don Bosco yanayopaswa kumwilishwa katika ulimwengu mamboleo mintarafu mikakati ya shughuli za kichungaji inayotekelezwa na Wanashirika wa Don Bosco kwa vijana, kwa kuwasaidia kuwa na mikakati ya maisha ya ujana na miito yao.

Padre Pascual Chavez anawataka Wasalesiani kuwa makini zaidi kwani watu na historia imebadilika, kiasi kwamba, haishangazi siku hizi kuona hata Wakristo wenyewe wanaishi kwa kubabaisha. Ni mwaliko kwa Wasalesiani kuwaendea na kuwashirikisha karama na tasaufi yao vijana kutoka dini na madhehebu mengine, ili wao pia waweze kuguswa na tasaufi ya Don Bosco.

Padre Pascual Chavez anahitimisha dhima itakayoongoza Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 200 tangu alipozaliwa Mtakatifu Don Bosco; Awamu ya Mwaka wa Tatu kwa kukazia: mang’amuzi ya maisha ya kiroho ya Mtakatifu Don Bosco; dhamana ya kuishi upendo katika shughuli za kichungaji sanjari na kuwashirikisha wengine Tasaufi ya maisha ya Wasalesiani watu wenye miito mbali mbali na kwamba, kiwe ni kipindi cha kujisomea Maandiko ya Mtakatifu Don Bosco.








All the contents on this site are copyrighted ©.