Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mwambata wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji
wa watu na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya Kazi za Kimissionari katika mahojiano na
Radio Vatican anafafanua baadhi ya changamoto ambazo Kanisa linakabiliana nazo katika
azma ya Uinjilishaji mpya kwa sasa.
Utandawazi
na athari zake ni kati ya changamoto kubwa zinazolikabili waamini wengi, lakini hasa
zaidi wale wanaotoka kwenye nchi ambazo zilibahatika kusikia kwanza Habari Njema ya
Wokovu ikitangazwa kwao, lakini sasa wamekengeuka kiasi kwamba, wanataka kumn'goa
Mwenyezi Mungu kutoka katika maisha na vipaumbele vyao. Huu ni mwanzo wa kuporomoka
kwa misingi bora ya maisha ya kiroho, kiutu na kimaadili. Uinjilishaji mpya ni mwaliko
kwa waamini kumpatia Kristo kipaumbele cha kwanza katika maisha yao ya kila siku.
Askofu
mkuu Rugambwa anaendelea kusema kwamba, Nchi zile ambazo zilikuwa na Mapokeo na Utamaduni
wa Kikristo, zikawa mstari wa mbele kutuma idadi kubwa ya Wamissionari kwenda sehemu
mbali mbali za dunia kwa ajili ya kutangaza Injili ya Kristo, leo hii zinakabiliwa
na uhaba mkubwa wa Wahudumu wa Injili. Hii ni changamoto kwa Makanisa ya zamani kushirikiana
kwa hali na mali na Makanisa ya Kimissionari katika mikakati ya kichungaji, ili kusaidia
kupunguza uhaba wa wachungaji unaoendelea kujitokeza hasa katika nchi za Ulaya.
Ukata
wa fedha kwa ajili ya kugharimia mchakato wa Uinjilishaji ni kati ya changamoto ambazo
zinajitokeza kwa sasa. Askofu mkuu Protase Rugambwa anasema, Mashirika ya Kipapa ya
kazi za Kimissionari yana jukumu la kumsaidia Baba Mtakatifu kutekeleza wajibu wake
barabara ndani ya Kanisa. Mashirika haya yamekabidhiwa dhamana ya kuhamasisha, kukuza
imani na kumtangaza Kristo katika medani mbali mbali za maisha.
Hili ni jukumu
ambalo linawashirikisha waamini na watu wote ili kuweza kuchangia kwa hali na mali.
Takwimu za miaka kumi iliyopita zinaonesha kwamba, mchango wa raslimali fedha kutoka
kwa waamini kwa ajili ya kugharimia shughuli za Uinjilishaji umepungua kwa kiasi kikubwa.
Mwelekeo huu kwa kiasi kikubwa unachangiwa na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.
Hizi ni baadhi ya changamoto zinazopaswa kufanyiwa kazi ili mchakato wa Uinjilishaji
uendelee kushika kasi katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.