2013-08-16 07:20:37

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 20 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Mpendwa ninakukaribisheni katika safari ya tafakari Neno la uzima kadiri tulivyojaliwa na Mama Kanisa. Leo tunasafiri pamoja katika Dominika ya 20 ya Mwaka C wa Kanisa. RealAudioMP3

Ujumbe wa furaha na wa kukujalia maisha ni kwamba, Bwana amekuja kuleta moto duniani. Moto huo ni Roho Mtakatifu. Tunaanza kufikiria maramoja zawadi ya Pentekoste. Hivi kama moto huo usingetupwa duniani, Kanisa lingekuwaje sasa, Bwana ajua lakini lingekuwa pengine limezimika, bila maisha, bila maisha ya mbele! Moto wa Injili kama nilivyokwisha ni Roho wa Mungu, ni mapendo ya Mungu, ni maisha hai.

Mpendwa, kama Injili inaadhimisha huo moto wa upendo basi kwa vyovyote vile maisha hayawezi kutafsiriwa kama maisha ya kujifurahisha bali maisha ya huduma kwa waliowahitaji.

Ndiyo kusema, tunapata ujumbe huo katika maneno ya Bwana mwenyewe sikuja kuwafanya mkakae kwa amani bali nimekuja kuwatingisha na kuwashitua ili mkawajibike katika kujenga maisha ya kumwelekea Mungu.

Bwana anaendelea katika Injili kutoa maneno mazito ambayo tusipokuwa waangalifu twaweza kupotea. Anasema nimkuja kuleta utengano na mafarakano. Katika hali ya kawaida kuna utengano kulingana na itikadi, rangi, umri nk. Bwana hazungumzii hayo bali ataka kutufundisha kuwa ulimwengu huu haundeshwi kwa mantiki tu ya kibinadamu bali kwa moto wa Pentekoste, moto wa Injili ambao huzigonga dhamiri zetu. Moto ambao huwasha mapendo ya mioyo yetu ili yaweze kuendana na safari ya wokovu ambayo hujitokeza kwa njia ya Jumuiya. Moto huu hutaka tufikirie juu ya mambo ya uzima wa milele badala ya kufikiria mambo ya kawaida.

Mpendwa msikilizaji wa radio Vatican, kama moto huu ukikolea katika maisha ya watu basi huweza pia kufika katika familia zetu na kuwasha mwanga ambao waweza kujenga utengano kwa namna moja au nyingine. Katika Kanisa, Jumuiya ya waamini wapo ambao wameupokea moto huo moja kwa moja na hivi wanakuwa chanzo cha maisha ya kujitoa kikamilifu kwa ajili ya wengine. Hali hii yaweza kuzaa kutoelewana na hasa kwa wale wasio na imani. Hata hivyo yatupasa kutambua kuwa Upendo ambao ndio moto unaotupwa duniani huvumilia na kuyaona yote katika jicho la Bwana kadiri ya Mtakatifu Paulo.

Barua kwa Waebrania yatufundisha kusadiki kina na kuvumilia mateso yatakayotoka na moto uliotupwa duniani na Bwana. Mfano wa uvumilivu ni watakatifu, wafiadini na hasa Bwana wetu Yesu Kristo aliyekubali kuteswa hadi kufa Msalabani. Jambo hili linampata Yeremia katika Somo la Kwanza anapotumwa kuwaambia Wayahudi kuwa mji wa Yerusalemu utatekwa, basi wakuu wanachukia na kukamata na kumtupa katika shimo kuu. Kwa huruma ya Mungu anaokolewa katika taabu hiyo. Basi nasi katika kuishi imani yetu kwa hakika kutakuwa na taabu ambazo tunahitaji kuzivumilia.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, pengine nyakati hizi kuna mashahidi na waungama dini wengi wanaoendelea kutoa maisha yao kwa ajili ya ushuhuda kwa Kristo na Kanisa lake, kuliko wakati ule wa Kanisa la Mwanzo.

Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii inaletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.