2013-08-16 07:41:07

Miaka 110 ya kuzaliwa kwa mtetezi wa wagonjwa wa ukoma duniani!


Jumuiya ya kimataifa tarehe 17, Agosti 2013 inaadhimisha siku ya 110 ya kuzaliwa kwa mtume wa waathirika wa ugonjwa wa ukoma Raoul Follereau aliyezaliwa Nevers, Ufaransa tarehe 17 Agosti 1903 na kuaga dunia mjini Paris, Ufaransa, tarehe 6 Desemba, 1977. RealAudioMP3

Raoul alikuwa ni mwanzilishi wa chama cha Raoul Follereau ambacho kinasaidia na kuwatetea waathirika na wagonjwa wa ukoma, na hasa kwenye nchi za kiafrika. Mtazamo wa Kikristo uliomwezesha Follereau kufanya kazi hii na nyinginezo kwa mapendo ulikuwa chanzo cha kuanzishwa maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Wagonjwa wa Ukoma iliyofanyika kwa mara ya kwanza Januari 1954.

Ili kumkumbuka mtume huyu wa waathirika wa ukoma, Jumuiya ya kimataifa imeandaa namna mbalimbali za kuadhimisha Siku hii kwa mwaka 2013. Ramsha ramsha hizo zitafanyika nchini Ufaransa na kwingineko duniani, mojawapo ikiwa ni kutolewa kwa stempu ya kipekee na Kitengo cha Posta cha Mji wa Vatican.

Mtume Raoul Follereau alizaliwa huko Nevers, Ufaransa mnamo 1903. Akiwa bado kijana mdogo alipata kuvuma kwenye magazeti ya Ufaransa kama mwandishi wa habari na mtunzi stadi wa mashairi. Katika moja ya safari zake Barani Afrika kama mwandishi wa habari, akiandika juu ya maisha na huduma za Padre Charles De Foucauld kwenye maandalizi ya maadhimisho ya miaka 20 tangu kifo cha Padre huyo, kijana Raoul Follereau alikumbana ana kwa ana na waathirika wa ugonjwa wa ukoma.

Tukio hili lilimgusa sana rohoni na akilini mwake na hivyo kubadili maisha yake moja kwa moja kadiri ya mwanga wa imani. Huu ukawa ndio mwanzo wa safari yake ya kuwahudumia na kutetea haki za waathirika wa ugonjwa wa ukoma, akisaidiana na mkewe Madelaine Boudou.

Kwa miaka kumi iliyofuata Raoul Follereau aliizunguka dunia akiongoza mikutano na semina zaidi ya elfu moja ambayo ilimsaidia kuchangisha fedha za kuanzisha Hospitali ya waathiriwa wa ukoma mjini Adzope, nchini Ivory Coast. Leo hii Hospitali hiyo inajulikani kama Taasisi ya Kitaifa ya Kutibu Ukoma R. Follereau.

Hata hivyo, Raoul Follereau hakuridhika na kuwa tu na Hospitali kwa ajili ya matibabu, msukumo wa mapendo kutoka ndani ya roho yake ulimtaka pia kuhakikisha kuwa waathirika wa ugonjwa wa Ukoma hawabaguliwi wala kutengwa na jamii kama ilivyokuwa ikitokea, jambo ambalo liliwakosesha furaha wagonjwa hao kwani hawakujitakia ugonjwa huo.

Alitumia uwezo wake kama Mwandishi kuandika juu ya ugonjwa wa Ukoma na kulijulisha Shirika la Afya Duniani kwamba, ukoma ni ugonjwa kama ugonjwa wowote ule wa kuambukiza, ulikuwa na tiba, sio ugonjwa wa kurithi, na kwamba haikuwa vyema kuwatenga waathiriwa wa ugonjwa huo.

Tarehe 20 mwezi Septemba 1952, Raoul Follereau aliuomba Umoja wa Mataifa kuanzisha mkataba ambao ungeweka wazi sheria kuhusiana na ugonjwa wa ukoma na kuhakikisha ulinzi wa haki za waathirika na kuwatoa kwenye jela ya kihisia walimokuwa wamefungwa kwa kutengwa na jamii. Ombi hili lilikubalika hapo 1954, miaka miwili baadaye, kwenye kikao cha kitaifa cha Ufaransa. Ni katika mwaka huu pia ambapo Umoja wa Mataifa ulianzisha Siku ya Ugonjwa wa Ukoma Kimataifa.

Lengo ni kuhakikisha kwamba, waathirika, sawa na wagonjwa wengine wote, wanapata fursa ya kutibiwa na kuheshimiwa kama binadamu. Zaidi ya hilo, alikuwa pia na lengo la kuiponya jamii kutokana na woga kuhusu ugonjwa wa ukoma uliojiri sana nyakati hizo sehemu mbali mbali za dunia.

Leo hii siku hii inaadhimishwa na zaidi ya mataifa 150 kote duniani; ni maadhimisho yanayoashiria kukamilika kwa lengo la mwanzilishi wa siku yenyewe, ambaye alitamani sana kuona mshikamano wa kimapendo na furaha kwa wagonjwa wote wanapochukuliwa kama binadamu, kitu ambacho ni cha kujivunia, kwani thamani yake ni kubwa zaidi kuliko misaada yoyote ile inayoweza kutolewa.

Jumuiya ya kimataifa inapoadhimisha miaka 110 ya kuzaliwa kwake mtume huyu wa Waathirika wa Ugonjwa wa ukoma inajivunia mchango wake uliotokana na bidii, ujasiri, na msukumo wa upendo wa Kikristo. Ni changamoto kwao wakristu wa kizazi kipya kuitunza tunu hii inayojidhihirisha pale Yesu Kristo mwenyewe alipoyatoa maisha yake na kufa msalabani kwa ajili ya nduguze.

Leo hii kuna vyama na mashirika yaliyoenea kote duniani kumuenzi Raoul, na kuendeleza huduma kwa maskini na wale waliosukumizwa pembezoni mwa jamii. Vyama hivi ni kama kile cha Marafiki wa Raoul chenye matawi kama vile Italia, India na Ufaransa. Marafiki wa Raoul Follereau pia wako katika nchi kadhaa za kiafrika kama vile Msumbiji, Ivory Coast, Togo, Congo, Sudan, Rwanda, Burundi, Tanzania na Angola.

Wakati wa uhai wake, Raoul Follereau alipata, kuandika vitabu kadhaa juu ya mapendo kama vile: “Bila Wewe Hakuna Mapendo; Fanya Maisha yetu yang’ae Upendo; na zaidi alimwomba Mungu kuwaponya binadamu na ukoma wa kweli ambao ni kumsulubu Yesu kwa kutowajali ndugu zake waathirika wa ugonjwa wa Ukoma. Ni mfano kwa wote wale wanaopania kumfuata Yesu Kristo kwa vitendo sanjari na kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya mafao ya wengi.


Makala hii imeandaliwa na
Sr. Bridgida Samba Mwawasi,
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.