Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni anaungana na viongozi
wengine kutoka katika Jumuiya ya Kimataifa kulaani mauaji ya watu wasiokuwa na hatia
yanayoendelea kupamba moto nchini Misri. Anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi
mema kusali kwa ajili ya kuombea mchakato wa uponyaji, haki na amani miongoni mwa
wananchi wote wa Misri.
Ni jambo la msingi ikiwa kama wananchi wote wa Misri
watakuwa na haki sawa na dhamana pamoja na wajibu wa kusimama kidete kulinda na kudumisha
mafao ya wengi. Wananchi wa Misri wakubali tofauti zao za kisiasa na kidini kama changamoto
ya kujenga na kuimarisha umoja na mshikamano wa kitaifa. Baraza la Makanisa Ulimwenguni
linasikitishwa sana na wimbi la uchomaji wa Makanisa unaofanywa na baadhi ya waamini
wenye misimamo mikali ya kiimani.
Kuanzia mwaka 2011 Misri imeendelea kukabiliana
na machafuko ya kijamii hali ambayo bado inaendelea kusababisha maafa makubwa. Umefika
wakati kwa wananchi wa Misri kusahau tofauti zao za kisiasa na kidini na kuanza kutafuta
misingi ya haki, amani na upatanisho; ili kwa pamoja waweze kukabiliana na changamoto
zinazojitokeza mbele yao. Ni matumaini ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni kwamba, vita
inayoendelea nchini Misri haitatafsiriwa kuwa ni vita kati ya Waamini wa dini ya Kiislam
na Kikristo. Viongozi wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni wanaendelea kuungana na watu
wenye mapenzi mema kwa ajili ya kuombea amani na utulivu.
Taarifa ya Wizara
ya Afya inaonesha kwamba, hadi kufikia tarehe 15 Agosti 2013, zaidi ya wananchi 623
wamekwishapoteza maisha kutokana na mashambulizi yanayoendelea kujitokeza sehemu mbali
mbali nchini Misri. Pengine idadi hii ikaongezeka maradufu.
Viongozi mbali
mbali wa Jumuiya ya Kimataifa wamelaani mauaji ya raia wasiokuwa na hatia yanayoendelea
nchini Misri. Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bwana Ban Ki-Moon amelaani matumizi
makubwa ya nguvu za kijeshi dhidi ya raia. Jumuiya ya Kimataifa kwa sasa ina wajibu
wa kuhakikisha kwamba, inajitahidi kuzuia ili Misri isitumbukie katika vita ya wenyewe
kwa wenyewe ambayo itasababisha maafa makubwa!