2013-08-14 11:08:37

Waamini wanamsubiri Papa Francisko Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo kwa Ibada ya Misa, tarehe 15 Agosti 2013


Katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Kupalizwa Mbinguni mwili na roho inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila Mwaka ifikapo tarehe 15 Agosti, Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Ikulu Ndogo ya Castel Gandolfo, iliyoko nje kidogo ya mji wa Roma. Mara baada ya Misa, Baba Mtakatifu atasali Sala ya Malaika wa Bwana, na waamini pamoja na mahujaji watakaokuwa wamefika mjini Castel Gandolfo.

Kabla ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, Papa Francisko anatarajiwa kuwatembelea Watawa wa ndani wa Mtakatifu Klara wanaoishi hapo mjini Castel Gandolfo. Hii ni Monasteri iliyojengwa kunako mwaka 1631. Ikabomolewa wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia, hali ambayo iliwalazimisha Watawa waliokuwa wanaishi kwenye Monasteri hii kuhamishiwa mjini Roma.

Katika kipindi hiki, Kanisa kwa namna ya pekee linamkumbuka Marehemu Sr. Maria Chiara Damato aliyefarkki dunia hapo tarehe 9 Machi 1948 kwa ugonjwa wa Kifua Kikuu. Tayari mchakato wa kumtangaza kuwa Mwenyeheri unaendelea baada ya mwili wake kufukuliwa kunalo tarehe 22 Novemba 1999 na kukutwa bado haujaharibika.

Watawa wanaoishi kwenye Monasteri hii wanautumia muda wao mwingi kwa ajili ya: Sala, Tafakari na Kazi. Wanawasaidia waamini katika Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu, katika Kikanisa ambacho kiko wazi kwa ajili ya wageni kutoka nje. Ni watawa ambao wamebobea katika kazi za mikono na matunda ya kazi za mikono yao wanagawana na maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kadiri ya ufukara wa Mtakatifu Klara wa Assisi.

Itakumbukwa kwamba, kwa mara ya kwanza Monasteri hii ilitembelewa na Papa Paulo wa sita hapo tarehe 3 Septemba 1971, ili kuwashirikisha matunda ya Mababa wa Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican kuhusu umuhimu wa kufuata Katiba, maisha ya Kijumuiya, Nadhiri na kwamba, kama watawa walikuwa ni alama ya matumaini ya Kanisa.

Tarehe 14 Agosti 1979, Mwenyeheri Yohane Paulo II aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Monasteri hii na kuwaomba Watawa hao kuendelea kusali kwa ajili ya mafao ya binadamu wote na kwamba, Kanisa linawaangalia kwa jicho la matumaini katika maisha yao yaliyojificha machoni pa binadamu, lakini Mwenyezi Mungu anasikiliza sala na sadaka yao.

Ilikuwa ni tarehe 15 Septemba 2007, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, alipokutana na kuzungumza na watawa wanaoishi katika Monasteri hii, akiwataka kuwa ni vielelezo vya moto wa upendo na sala kwa ajili ya kumwombea Khalifa wa Mtakatifu Petro, ili aweze kutekeleza dhamana na wajibu wake aliokabidhiwa na Kristo mwenyewe kwa ajili ya Kanisa lake.

Aliwakumbusha kwamba, wao ni warithi wa tunu msingi za Kiinjili na amana iliyoachwa na Mtakatifu Francisko wa Assisi na Mtakatifu Klara, waliojitoa kimasomaso kwa ajili ya Mungu na Jirani, wakaishi Nadhiri na wakaonesha heshima ya kulinda na kutunza mazingira.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI aliwataka watawa hao kuonesha ile furaha ya Injili katika hali ya ukawaida pasi na kupenda makuu, kwa kutambua kwamba, wanatekeleza dhamana na utume wa Kanisa katika ari na mwamko wa kimissionari. Alisema kwamba, ni matumaini yake kuwa Mwenyezi Mungu ataendelea kuwaita wasichana wengi na watakatifu wanaotaka kujitoa kwa ajili ya Mungu na jirani katika maisha ya utawa!







All the contents on this site are copyrighted ©.