2013-08-14 09:16:00

Chuo Kikuu cha SAUT na mikakati ya kupambana na ujinga Afrika Mashariki


Askofu Bernardin Mfumbusa wa Jimbo Katoliki Kondoa aliyewahi kuwa mkuu wa taaluma Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino cha Tanzania, SAUT, katika makala iliyoandikwa kwenye Gazeti la L'Osservatore Romano linalomilikiwa na Vatican anasema kwamba, Chuo Kikuu cha SAUT ni kati ya matunda ambayo Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linajivunia katika mikakati yake ya Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania limewekeza kwa kiwango cha juu katika sekta ya elimu kwa lengo la kutaka kumkomboa mtanzania kutoka katika lindi la ujinga, maradhi na umaskini. Chuo Kikuu cha SAUT kilichoanzishwa rasmi kunako Mwaka 1998, kimekuwa ni kitovu cha majiundo ya kiakili, kiroho, kimwili na kimaadili kwa vijana kutoka ndani na nje ya Tanzania. SAUT inapania kuwajengea uwezo wanafunzi wake ili waweze kutoka kifua mbele kwa ajili ya kuwatumikia wananchi wenzao kwa ari kubwa, majitoleo, taaluma na uzalendo.

Askofu Mfumbusa anasema kwamba, SAUT katika kipindi chote hiki imeendelea kujitanua na kwa sasa ni kati ya Vyuo Vikuu Barani Afrika vyenye idadi kubwa ya wanafunzi. SAUT inaendelea kupokea wanafunzi kutoka Burundi, Rwanda, Malawi, Uganda, DRC, Kenya, Zambia, Sudan, Ethiopia, Eritrea, Ujerumani na Finland. Majaalim wake wengi licha ya kuwa ni watanzania, lakini pia kuna mchango wa Jumuiya ya Kimataifa kutoka katika baadhi ya nchi za Kiafrika kama vile Benin, Kenya na Ulaya.

Askofu Mfumbusha anasema, licha ya SAUT kutoa taaluma kwa kuzingatia viwango vya kimataifa, lakini pia inakazia masuala ya maadili na utu wema, ili kuwafunda wanafunzi watakaowajibika barabara mbele ya Mwenyezi Mungu na Jamii inayowazunguka. Rushwa na ufisadi ni kati ya matatizo makubwa yanayoikabili Tanzania.

Kumbe, anasema Askofu Mfumbusa, ikiwa kama vijana hawatapewa misingi bora ya maadili na utu wema, uzalendo na sadaka; ukweli na uaminifu, wanaweza kujikuta kwamba, wanatumbukia au kutumbukizwa kwenye dimbwi la rushwa na ufisadi, kwa ajili ya kupata utajiri wa haraka haraka pasi na jasho.

Kanisa Katoliki nchini Tanzania linapenda kushiriki kikamilifu katika kuchangia ustawi na maendeleo ya watanzania wengi, kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa Bara la Afrika linalopania kujitegemea na kuwategemeza watu wake kwa hali na mali. Chuo Kikuu cha SAUT kinaendelea kuongeza vitivo kwa kusoma alama za nyakati na mahitaji ya maendeleo ya sayansi na teknolojia kwa wakati huu. Chuo kinaendelea kuboresha maktaba zake ambazo ni chemchemi ya ufahamu na hosteli kwa ajili ya wanafunzi wanaotoka mbali.

Wanafunzi wa Kitivo cha Mawasiliano ya Jamii wanayo fursa ya kufanya mazoezi kwenye Kituo cha Radio SAUT na Kituo cha Televisheni kinachoendeshwa na kusimamiwa na wanafunzi wenyewe.

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania kutokana na sera makini, moyo wa uzalendo na hali ya kujitosa kikamilifu bila ya kujibakiza, kunawawezesha kuendelea kutekeleza mikakati ya kuitanua SAUT ili iweze kuwa karibu zaidi na wanafunzi wake ndani na nje kwa kufungua Vyuo vishiriki mipakani mwa Tanzania. Askofu Mfumbusa anasema, Chuo Kikuu cha SAUT ni matunda ya mikakati ya shughuli za kichungaji kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Tanzania na Afrika kwa ujumla.







All the contents on this site are copyrighted ©.