2013-08-14 10:31:43

AMECEA kukutana Lilongwe kuanzia tarehe 16 hadi 26 Julai 2014


Uinjilishaji Mpya kwa njia ya wongofu wa ndani na ushuhuda wa imani ya Kikristo ndiyo kauli mbiu itakayoongoza Maadhimisho ya Mkutano wa 18 wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki na Kati, AMECEA, utakaofanyika nchini Malawi, kuanzia tarehe 16 hadi 26 Julai 2014.

Itakumbukwa kwamba, kunako Mwaka 2011, AMECEA iliadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu ilipoanzishwa wakati nchi nyingi za Kiafrika zikiwa katika vuguvugu la kudai uhuru wa bendera. Uimarishaji wa Jumuiya Ndogo ndogo za Kikristo kama shule ya Neno la Mungu, Maisha ya Kisakramenti, Matendo ya Huruma na Majiundo makini ya imani, zilipewa msukumo wa pekee na AMECEA katika uhai wake.

AMECEA imeona na kukabiliana na changamoto mbali mbali zilizokuwa zinajitokeza miongoni mwa wananchi wanaounda nchi za AMECEA katika elimu, afya na maendeleo endelevu. Kunako Mwaka 1976, AMECEA katika mikakati yake ya shughuli za kichungaji ikaamua kuanzisha Chuo Kikuu cha Kikatoliki Afrika Mashariki na Kati, CUEA.

Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino cha Tanzania, SAUT ni matunda ya changamoto za Mababa wa AMECEA. Hadi leo hii, AMECEA inaendelea kucharuka katika masuala ya maisha ya kiroho, elimu, afya na maendeleo ya Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.