2013-08-13 09:18:11

Nchi ya Ghana iko njia panda!


Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana linawataka waamini na wananchi wenye mapenzi mema kuendelea kudumisha misingi ya haki, amani, utulivu, upendo na mshikamano wa kitaifa, wakati huu Mahakama kuu inapojiandaa kutoa hukumu ya rufaa ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika nchini humo Desemba, 2012.

Kwa mara ya kwanza katika historia ya Ghana, Mahakama kuu imekubali kusikiliza rufaa iliyotolewa na vyama vya upinzani vilivyokataa kukubali matokeo ya uchaguzi mkuu nchini humo yaliyokuwa yamempatia ushindi Rais John Dramani Mahama. Mahakama ilianza kusikiliza kesi hii ya kihistoria tangu tarehe 16 Aprili 2013 na kumaliza kukusanya ushahidi wote hapo tarehe 17 Julai 2013. Mahakama kuu inatarajiwa kutoa hukumu ya kesi hii mwishoni mwa Mwezi Agosti 2013.

Baraza la Maaskofu Katoliki katika mkutano wake uliohitimishwa hivi karibuni, linawataka wananchi katika kipindi hiki kigumu na tete kujenga na kuimarisha amani na mshikamano wa kitaifa kwani ikiwa kama hawataweza kuwa makini, maafa makubwa yanaweza kutokea nchini Ghana. Amani na utulivu vidumishwe kabla, wakati na baada ya Mahakama kuu kutoa hukumu ya kesi hii ya kihistoria, inayoiweka Ghana katika njia panda.

Maaskofu Katoliki Ghana wanaendelea kuwahimiza waamini na wananchi katika ujumla wao, kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika ujenzi wa misingi ya haki, amani, utulivu na upatanisho wa kitaifa. Itakumbukwa kwamba, Ghana ilifanya marekebisho ya Katiba yake kunako mwaka 1992 na imeongoza chaguzi kuu mara sita na kwa mara ya kwanza, matokeo ya uchaguzi mkuu yamepingwa Mahakamani, kielelezo cha ukomavu wa kisiasa na kidemokrasia.

Katika hali hii tete nchini Ghana, vyombo vya mawasiliano ya Jamii vina mchango mkubwa wa kuhakikisha kwamba, vinasaidia mchakato wa kuimarisha amani, upendo, mshikamano na upatanisho wa kitaifa. Vyombo vya ulinzi na usalama vitekeleze wajibu wake kwa ajili ya mafao ya wengi. Kwa wale watakaobahatika kutangazwa kuwa ni washindi, watambue dhamana na changamoto iliyoko mbele yao katika ujenzi wa demokrasia shirikishi, wajibu na dhamana ya kusimama kidete kupambana na rushwa, ufisadi na ukosefu wa fursa za ajira miongoni mwa vijana, kwani haya ni kati ya matatizo makubwa yanayowakabili wananchi wa Ghana kwa wakati huu.

Maaskofu Katoliki Ghana wanasema, kwamba, amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomshikirisha mwanadamu. Wananchi hawana budi kuhakikisha kwamba, wanajifunza namna ya kulinda na kutunza zawadi ya amani kwa ajili ya mafao na ustawi wa nchi yao. Ni matumaini ya Baraza la Maaskofu Katoliki Ghana kwamba, Mahakama kuu itatekeleza wajibu wake kwa kuzingatia misingi ya ukweli na haki wakati wa kutoa hukumu.







All the contents on this site are copyrighted ©.