2013-08-13 07:48:15

Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Miaka 850 ya Kanisa kuu Notre Dame, Paris


Kardinali Andrè Vingt Trois, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Paris, Ufaransa anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kilele cha Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 850 tangu kujengwa kwa Kanisa kuu la Notre Dame, Jimbo kuu la Paris sanjari na Siku kuu ya Kupalizwa mbinguni Bikira Maria, hapo tarehe 15 Agosti 2013. RealAudioMP3

Sherehe hizi zinatanguliwa na siku mbili za Maadhimisho, kuanzia tarehe 14 Agosti 2013 kwa Maandamano makubwa ya mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Katika mkesha wa Siku kuu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni, majira ya jioni waamini na mahujaji watafanya maandamano kwenye Meli, Boti na Mashua kuzunguka Mto Senna, ulioko mjini Citè na St. Louis.

Waamini na mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia watapata fursa pia ya kuangalia maonesho ya picha zilizochorwa kunako karne ya XVII, kuhusiana na maisha ya Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa. Picha hizi zimeendelea kuhifadhiwa kwenye Kanisa kuu la Notre Dame, Jimbo kuu la Paris kutokana na utashi ulioneshwa na Mfalme Louis XIII aliyeiweka nchi ya Ufaransa chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria kunako mwaka 1638.








All the contents on this site are copyrighted ©.