2013-08-13 08:19:20

Jubilee ya miaka 200 ya kukamilika kwa Ujenzi wa Kanisa kuu la Jimbo kuu la Mexico City


Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Kardinali Norberto Rivera Carrera wa Jimbo kuu la Mexico City, nchini Mexico, wakati huu wanapoadhimisha Jubilee ya miaka 200 tangu kukamilika kwa ujenzi wa Kanisa kuu Jimboni humo, hapo tarehe 15 Agosti 2013, anasema, ni changamoto kubwa ya kukuza ari na mwamko wa kimissionari. Waamini watumie fursa hii kuimarisha imani, matumaini na mapendo na vijana waendelee kufurahia zawadi ya imani.

Baba Mtakatifu anawaambia waamini wa Jimbo kuu la Mexico City kwamba, Maadhimisho ya Jubilee hii yanafumbata utajiri na amana kubwa ya maisha ya kiroho. Iwe ni fursa ya toba na wongofu wa ndani, kila mwamini akijitahidi kutekeleza dhamana na wajibu wake katika maisha na utume wa Kanisa kama Mbatizwa, tayari kujitosa kimasomaso kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa ari na nguvu mpya ya kimissionari.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, waamini katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu wanajichotea nguvu ya kuweza kutolea ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake, kwa njia ya upendo kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Ni mwaliko wa kujenga na kuimarisha matumaini kwa ajili ya kesho iliyo bora zaidi bila kutoa mwanya kwa baadhi ya watu wanaotaka kupokonya matumaini haya kutoka katika mioyo ya waamini.

Baba Mtakatifu Francisko anawataka waamini wa Jimbo kuu la Mexico City, kuhakikisha kwamba, Neno la Mungu linalotangazwa wakati wa Ibada mbali mbali linajikita katika mioyo na maisha ya watoto na vijana ambao ni mlango wa furaha na matumaini kwa Kanisa na Jamii. Vijana wapewe na kurithishwa imani na tunu msingi za maisha ya Kikristo na kiutu, kwa kutambua kwamba, Yesu Kristo ni Mkombozi na Rafiki mwema, kamwe hawezi kuwaacha katika utupu!

Baba Mtakatifu anaendelea kuwahimiza wazazi na walezi kuhakikisha kwamba, wanatekeleza kwa dhati dhamana waliyokabidhiwa na Mama Kanisa na Jamii katika malezi na makuzi ya watoto wao, si tu kwa kutegemea nguvu zao binafsi bali pia kwa neema na baraka za maisha ya sala.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha ujumbe wake wa matashi mema wakati huu Jimbo kuu la Mexico City linapoadhimisha Jubilee ya miaka 200 tangu kukamilika kwa ujenzi wa Kanisa kuu la Jimbo kuu la Mexico City kwa kuwaweka waamini wote chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa Guadalupe.







All the contents on this site are copyrighted ©.