2013-08-12 12:19:20

Familia ina dhamana ya kurithisha imani ya Kikristo kwa watoto wake!


Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil, limeanza Maadhimisho ya Juma la Familia Kitaifa, litakalohitimishwa hapo tarehe 17 Agosti 2013 kwa kuongozwa na kauli mbiu "Urithishaji na elimu ya imani ya Kikristo katika Familia". Mababa wa mkutano mkuu wa Aparecida walibainisha kwamba, Familia ni kati ya zawadi kubwa ambayo Mwenyezi Mungu amewakirimia wananchi wa Amerika ya Kusini.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil wakati huu wa Maadhimisho ya Juma la Familia Kitaifa, anapenda kuchukua fursa hii kwanza kabisa kuwashukuru kwa mapokezi makubwa waliyomwonesha wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Brazil sanjari na Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani huko Rio de Janeiro.

Baba Mtakatifu anawaalika kwa namna ya pekee, wazazi na walezi kuhakikisha kwamba, wanatekeleza dhamana na utume wao ndani ya Familia, kwa kutambua kwamba, wao ni wadau wa kwanza wanaoshirikiana na Mwenyezi Mungu katika malezi na makuzi ya watoto wao kwa sasa na kwa siku za usoni. Kutokana na dhamana hii, wazazi na walezi wanayo dhamana kubwa ya kuhakikisha kwamba, wanajenga na kudumisha misingi ya imani kama sehemu ya mchakato wa ukomavu wa imani miongoni mwa watoto wao.

Wazazi na walezi walirthishe imani hii kwa njia ya maneno, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili na matakatifu; kwa kutambua na kuenzi kweli msingi za maisha kadiri ya upendo na mpango wa Mungu katika maisha ya mwanadamu; watoto wasaidiwe kupata mwanga na ufunuo wa Mungu katika hija ya maisha yao. Katika ulimwengu wa utandawazi usiojali wala kuguswa na mahangaiko ya jirani, wazazi wawasaidie watoto wao kutambua na kuthamini zawadi ya maisha inayopaswa kulindwa tangu pale mtoto anapotungwa mimba tumboni mwa mama yake hadi mauti ya kawaida yanapomfika kadiri ya mpango wa Mungu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, watoto ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba, Jamii inawajibu wa kuwatunza na kuwasaidia wazee katika safari ya maisha yao hapa duniani, kwani wazee ni amana ya Jamii, wanamiliki utajiri mkubwa na hekima ambayo wanapaswa kuwarithisha vijana wa kizazi kipya. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, Brazil itaendelea kusimama kidete kulinda na kutetea upendo unaorutubishwa kwa njia ya imani kama kito cha thamani kutoka kwa Mwenyezi Mungu.

Mwishoni, Baba Mtakatifu anazikumbuka na kuziombea Familia nchini Brazil kwa kuziweka chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa Aparecida.







All the contents on this site are copyrighted ©.