Baba Mtakatifu Francisko ameacha alama za kudumu alipokuwa Rio de Jenairo kwenye maadhimisho
ya Siku ya 28 ya vijana Duniani. Ndivyo anavyoandika kwenye mtandao wa Baraza la
Maaskofu Katoliki, Brazil, Kardinal Odilo Pedro Scherer, Askofu Mkuu wa Jimbo la Sào
Paolo.
Alama alizoacha
Baba Mtakatifu Francisko ni nyingi ila Kardinale Odilo Pedro anagusia hasa alama tatu
zilizopewa kipaumbele cha kwanza na Papa Francisko: vijana, maskini na Kanisa.
Kwanza
kabisa Vijana wa kizazi kipya ndio waliokuwa wahusika wakuu na sababu ya Baba Mtakatifu
Francisko kwenda Brazil, ambako alikwenda kama Baba wa vijana wote, ili kukutana na
kuwaonjesha mapendo, pamoja na kuendelea kuwatia moyo kusonga mbele kwa imani na matumaini
kwa Kristo na Kanisa lake. Nao vijana waliitikia mwito wake kwa furaha kuu, wakazijaza
barabara za Rio na ufuko wa Copacabana kwa furaha na imani – furaha iliyoje!
Na
kuhusu maskini, Baba Mtakatifu alionyesha mshikamano wake na wote wanaosukumizwa pembezoni
mwa jamii. Alionesha moyo wa heshima, ukarimu na hali ya kuguswa alipokuwa anazungumzia
kuhusu umaskini wa hali na kipato, unaoendelea kumwandama mwanadamu katika hija ya
maisha yake hapa duniani. Baba Mtakatifu alikazia umuhimu wa waamini na watu wenye
mapenzi mema kujenga na kudumisha mshikamano wa upendo.
Watu hasa waliguswa
na moyo wa kujali alioonesha Baba Mtakatifu kwa wagonjwa na wenye mateso hasa alipotembelea
hospitali na kitongoji duni cha Varginha. Aliwashukuru wananchi wa Brazil kwa moyo
wao wa ukarimu na makaribisho mazuri waliomuonesha na akawaomba kusimama kidete ili
kuweza kuyashinda matatizo ya kijamii yanayoikumba nchi yao.
Aliwaomba wote
waliokuwa wakimsikiliza waepukane na uchu wa mali na madaraka, kwani furaha ya kweli
haitokani na vitu alivyo nayo mtu, bali utu wake, furaha na amani ya ndani; hivyo
waongozwe na moyo wa kiasi pasi ya kupenda makuu!
Kuhusu Kanisa; anaendelea
kusema Kardinali Scherer kuwa, Baba Mtakatifu anaendelea kulihamasisha Kanisa kuwasikiliza
vijana wake ili liweze kuwafikishia Habari Njema ya Wokovu pamoja na ile furaha ya
imani.Baba Mtakatifu anaendelea kuwahimiza viongozi wa Kanisa kwenda pembezoni mwa
Jamii na maisha ya watu, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya na mwamko wa
kimissionari kwa nyakati hizi.