2013-08-10 09:19:12

Endelezeni thawabu mlizovuna wakati wa Mfungo mtukufu wa Ramadhani!


Waamini wa dini ya Kiislam nchini Tanzania wametakiwa kuutumia mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhani ulioisha kama darasa na kuendeleza mambo mema waliyokua wakiyafanya katika kipindi chote cha mfungo. Kauli hiyo imetolewa na Shekhe wa mkoa wa Dodoma, Mustapha Rajabu wakati alipokuwa akihutubia waumini wa dini hiyo katika ibada ya Siku kuu ya Id el Fitr iliyofanyika katika msikikiti wa Ghadafi kwenye Manispaa ya Dodoma.

Shekhe Rajabu alisema kuwa Waislamu hawana budi kuutumia mwezi wa Mfungo wa Ramadhani kwao kuwa kama semina ambayo imewawezesha kutenda mema na kuacha mabaya ambayo hayampendezi Mungu. Alisema kwamba, haitakuwa na maana yoyote kwao kama hawatayaendeleza mambo mazuri ambayo wamekua wakiyafanya katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Aidha ametoa wito kwa Waislam kote nchini Tanzania kuendeleza umoja na mshikamano uliopo na kujiepusha katika machafuko mbalimbali.

“Tuishi kwa amani na upendo na mshikamano watu wote bila ya kujali itikadi zetu au makabila” alisema Shekhe Rajabu. Amewaonya waamini wa dini hiyo kuacha kuitumia siku kuu hiyo kama sehemu ya kufanya maovu kupindukia kwani ni kinyume na mafundisho ya Mwenyezi Mungu. “Tusiitumie siku hii kufanya machafuko kama vile kulewa kupindukia bali tusherehekea siku hii kwa amani na upendo” alisema.

Naye Shakila Nurdin, aliwaomba waumini wenzake wa dini ya kiislamu nchini waienzi amani na mshikamano uliopo kama Mtume Mohamed (S.W.A) alivyohimiza katika vitabu vyake vitakatifu. “Amani ikipotea tutakao pata shida ni sisi akina mama na watoto hivyo na sisi tujitahidi kuhimiza amani kuanzia majumbani makanisani na misikitini” Alisema Shakila.

Hata hivyo aliwaasa vijana kuepuka kukaa vijiweni bali wajishughulishe na mambo ambayo yatawaletea maendeleo tofauti na ilivyo sasa ambapo wamekuwa wakiilaumu serikali bila ya wao kufanya jihada zozote za kujikwamua kihali na kiuchumi.








All the contents on this site are copyrighted ©.