2013-08-08 10:48:48

Papa Francisko atuma salam za rambi rambi nchini Argentina


Baba Mtakatifu Francisko amemtumia salam za rambi rambi Askofu mkuu Josè Luis Mollaghan wa Jimbo kuu la Rosario, lililoko nchini Argentina kutokana na kuporomoka kwa jengo ambalo limesababisha watu 12 kufariki dunia, wengine 60 kujeruhiwa vibaya na 16 hadi sasa hawajulikani waliko. Jengo hili limeporomoka baada ya kuvuja kwa gesi mapema juma hili.

Ujumbe wa Baba Mtakatifu umeandikwa kwa niaba yake na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican. Baba Mtakatifu Francisko anaonesha masikitiko na uchungu mkubwa na anapenda kuungana na wote wanaoomboleza msiba huu mkubwa kwa njia ya sala na sadaka yake. Anawaombea majeruhi ili waweze kupona haraka na kuendelea na shughuli zao za kila siku. Ujumbe huu wa Baba Mtakatifu umesomwa wakati wa Maandamano ya Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Gaetano, Msimamizi wa Argentina, hapo siku ya Jumatano, tarehe 7 Agosti 2013.







All the contents on this site are copyrighted ©.