2013-08-08 08:07:52

Mwanga wa matumaini kwa vijana kutoka Rio 2013


Karibu ndugu msikilizaji katika hema la vijana ndani ya studio za Radio Vatican Baada ya maadhimisho ya 28 ya siku ya vijana duniani, nahisi msukumo ndani ya moyo kushirikishana nawe au kukumbushana machahche ya muhimu yaliyojili Rio de Janeiro. RealAudioMP3
Hii ni kwa sababu ya jinsi alivyotugusa Baba Mtakatifu Fransisko kwa upendo mkubwa, na sababu ya upendo nilio nao kwako.
Natumaini wote mliokuwa Rio de Janeiro, Brazil mtakuwa mmekwishafika nyumbani. Pole sana kwa safari na uchovu, na hongereni kwa kukamilisha hija hiyo ya imani na matumaini. Naamini matunda mengi ya: Imani na Sakramenti; Marafiki na hata ya uchumba yatajionesha kwa wakati muafaka. Mimi nawaombea kila jema katika hija ya maisha ya ujana!
Nendeni ulimwenguni kote mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi wangu (Mathayo 28, 19). Maneno hayo ya Bwana Yesu kutoka Injili ya Mathayo, ndiyo yalikuwa mada, au kauli mbiu ya maadhimisho haya ya 28 ya vijana kimataifa. Tunapokwenda kuwafanya watu kuwa wanafunzi katika familia zetu, sehemu za kazi, mashuleni, na katika jamii kwa ujumla, kuna mambo yaliyogusa sana maadhimisho ya vijana na maneno ambayo Baba Mtakatifu Francisko kasisitiza.
Wakati wa Ibada ya Njia ya Msalaba Baba Mtakatifu Francisko katualika tuchukue maisha yetu na kila kitu tulichonacho tumpelekee Yesu Msalabani. Furaha yetu, taabu na mahangaiko yetu, mafanikio na kushindwa kwetu. Twende kwa Yesu yeye ambaye ametuamini na kutupa utume huu wa kutangaza Injili yake.
Tarehe 23 Julai, Siku ya kwanza tu alipowasili Rio, alisema kuwa Kristu katuamini vijana ndio sababu katukabidhi utume huu wa kuishuhudia Injili. Na ni matumaini yake Baba Mtakatifu Fransisko kuwa sisi vijana pia hatuogopi kumkabidhi Kristu maisha yetu.
Ujumbe huu unatukumbusha maneno ya Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika Misa yake ya kwanza ya utume wake kama khalifa wa Petro mnamo mwaka 2005, alisema: vijana msiogope kumwamini kristu kwani hachukui uhuru wenu wala chochote kutoka kwenu, badala yake anawapa kila kitu.
Katika madhabahu ya Bikira Maria wa Aparecida Baba Mtakatifu Francisko kakusisitiza kijana udumu katika matumaini, ujiachie na kuruhusu kushangazwa na Mungu sababu Mungu wetu ni Mungu wa ma suprise kwani amesheheni upendo na maajabu kemkem, pia kakusisitiza uishi kwa furaha, kwani ndivyo Mwenyezi kanuia tangu mwanzo wa uhai wetu, tuishi kwa furaha.
Weka bidii katika michezo na uchukue michezo kama sehemu ya kukua kimwili na kiroho na sio kujenga uadui na ugomvi kati ya watu. Kumbe, wakati wa michezo tuburudike na tujenge urafiki zaidi.
Alipotembelea Hospitali ya Mt. Francisko wa Assis aliwafariji wagonjwa wa afya ya akili na hasa wale walioathiriwa na dawa ya kulevya. Baba Mtakatifu Fransisko amelaani vikali matumizi haramu ya dawa za kulevya na anawaalika wote wanaofanya biashara hii kuacha ili kuepuka kuharibu maisha ya vijana.
Zaidi Baba Mtakatifu Francisko kakualika kuwaheshimu na kuwasikiliza wazee. Mwaliko huu kausisitiza kwa namna ya pekee, katika maadhimisho ya kumbukumbu ya watakatifu Yoakimu na Anna, babu na bibi wa Bikira Maria. Nuru hii tulioipokea pamoja na mema mengi yaliyojiri Rio de Jeneiro, tuipeleke ulimwenguni kote tulipo.
Napenda kukukumbusha pia kuwa maadhimisho yajayo ya siku ya 29 ya vijana kimataifa yatafanyikia Cracovia, Poland mnamo mwaka 2016, yaani miaka mitatu kuanzia sasa. Kumbe, anza maandalizi mapema ili uweze kushiriki maadhimisho hayo.
Sina la ziada, endelea kumshuhudia Kristo kwa maneno na matendo pamoja na kuendelea kuwafanya wengi kuwa wanafunzi wake. Mpaka kipindi kingine tena. Kutoka Studio za Radio Vatican, ni mimi mtumishi wa Altare ya Bwana, Padre Celestin Nyanda.








All the contents on this site are copyrighted ©.