Uwanja wa Jomo Kenyatta Kenya wafungwa kutokana na ajali ya moto!
Serikali ya Kenya siku ya Jumatano imelazimika kuufunga Uwanja wa Ndege wa Kimataifa
wa Jomo Kenyatta baada ya moto kutokea kwenye uwanja huo mapema Jumatano asubuhi na
hivyo kusababisha hasara kubwa. Hakuna mtu aliyejeruhiwa kutokana na kuzuka kwa moto
huo ingawa umesababisha usumbufu na hasara kubwa kwa wasafiri na wafanyabiashara ndani
na nje ya Kenya.
Uchunguzi wa awali unaonesha kwamba, moto huo umesababishwa
na milipuko miwili, kadiri ya taarifa iliyotolewa na Reuters. Serikali ya Kenya inaendelea
kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini chanzo cha moto huo ambao umesababisha usumbufu
kwa wasafiri na watalii wengi wakati huu wa msimu wa utalii kwa nchi za Afrika ya
Mashariki. Kutokana na moto huo mashirika kadhaa ya Ndege yamefuta safari zake kwenda
Kenya.