Shirika la kutetea uhai Tanzania linapinga dhana ya utoaji mimba!
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kimetoa taarifa ya nusu mwaka, Januari – Juni
2013 kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Tanzania. Kwa jumla taarifa ya kituo hicho
ni nzuri kwani imetokana na utafiti makini. Sisi katika Shirika la Kutetea Uhai [Pro-Life]
Tanzania tumepokea na kuunga mkono mengi yaliyotolewa na taarifa hiyo.
Hata
hivyo kipengele kinachohusu ‘haki ya kutoa mimba kiusalama’ [safe abortion] hatukubaliani
nacho na tunakipinga kwa nguvu zetu zote. Kwa bahati mbaya sana kipengele hicho kimetolewa
katika muktadha wa ‘haki ya kuishi’. Katiba ya Jamhuri wa Tanzania [1977], ibara ya
14 inasema, “Kila mtu anayo haki ya kuishi na kupata kutoka kwa jamii hifadhi ya maisha
yake…”
Ukizingatia ibara hiyo, jambo la kwanza tunalopaswa kulielewa ni tasfiri
ya ‘mtu’. Kwa kadiri ya tafsiri ya watetezi uhai, ‘mtu’ ni binadamu yeyote aliye hai.
Katika maumbile asilia, uhai wa mtu huanza tangu wakati wa kutungwa mimba na unadumu
hadi kifo chake cha kawaida. Kwa hiyo haki ya kuishi ni haki ya kila mtu, yule aliyezaliwa
na yule ambaye bado hajazaliwa.
Na kwa kweli mtu hawezi kuzaliwa, na kupata
haki ya kuishi, kama kwanza hakuwepo kabla yake akiwa hai. Ndiyo kusema, ‘mimba ni
binadamu [mtu] hai katika tumbo la mama. Mtu huyo, kwa hiyo, anayo “haki ya kuishi
na kupata kutoka kwa jamii hifadhi ya maisha yake…” Jamii inayomzunguka mtu [binadamu]
huyu ni kwanza wazazi wake, ndugu zake, majirani, taasisi mbalimbali na miundo ya
sheria na taratibu mbalimbali za kimila na za kiserikali.
Kila tumwonapo mama
mja mzito, mwenye mimba, tunafahamu kuwa wapo watu wawili – mama [mwanamke] mwenye
kubeba hiyo mimba, yaani mwenye mtu [binadamu] ndani ya tumbo lake na mtu [binadamu]
huyo ndani ya tumbo la mama yake. Kila mmoja kati ya hao wawili wana haki ya kuishi.
Mama ana haki ya kuishi na huyo aliyemo ndani ya tumbo lake ni mtu mwenye haki ya
kuishi sawa na mama yake. Hakuna mwenye haki zaidi kuliko mwingine. Wote wana haki
sawa ya kuishi na kupata kutoka jamii hifadhi ya maisha yao.
Haki ya kuishi
haitegemei sheria yoyote. Sheria zipo kwa sababu binadamu [watu] wapo. Kwa hiyo siyo
sahihi kuufaya uhai wa mtu utegemee sheria kama inavyosema Katiba ‘kwa mujibu wa sheria’.
Uhai wa mtu upo hata kama sheria haipo. Na katika historia binadamu alianza kuishi
kabla ya kuwepo kwa sheria. Sheria zilikuja ili kuweka utaratibu na kuwezesha mahusiano
bora ya kibinadamu na kulinda amali za jamii na taifa.
Maana ya kutoa mimba
ni ipi? Hata kama hutaki kukubali, ukweli msingi utabaki kuwa, ‘kutoa mimba maana
yake kumwua kwa makusudi binadamu [mtu] ambaye bado hajazaliwa’, yaani, aliyemo katika
tumbo la mama, kwa ajili ya kutimiza hamu ya kusudio fulani. Na tukimwangalia mtu
[binadamu] katika mgawanyo wa kirika; yaani, utoto, ujana, utu-uzima na uzee, mtu
aliyemo katika tumbo la mama ni mtoto mdogo, aliye hai ambaye ameanza safari ya kuishi
wake kuelekea hatua nyingine za kuzaliwa, utoto, ujana, utu-uzima na uzee.
Umri
wako wa leo unahesabika tangu siku ile ya kutungwa mimba, na wala sio tangu siku ya
kuzaliwa kama ambavyo wanadamu wamejidanganya. Siku ya kuzaliwa ni moja ya matukio
muhimu katika uhai wa binadamu. Nataka kusema kuwa, huwezi kuwepo leo, kama hukuwapo
kwanza katika tumbo la mama yako, ambapo ulijulikana kama ‘mimba’. Kumbe, kama mama
yako angeamua ‘kutoa mimba’, yaani kukuua wewe ulipokuwa mimba, usingalikuwapo leo.
Haki
ya kutoa mimba kiusalama maana yake nini? Kwa kadiri ya mashabiki na watetezi wa vitendo
vya utoaji mimba, utoaji mimba salama humaanisha kuwa, wakati mtoto anauwa katika
tendo la utoaji mimba, mama yake anakuwa salama, ikimaanisha kuwa hapati madhara wala
hafi. Lakini je, upo utoaji mimba salama? Wanazuoni mbalimbali waliobobea katika taaluma
ya mimba wanatujulisha kuwa hakuna utoaji mimba ulio salama.
Katika kila kitendo
cha utoaji mimba, mmoja anauawa, mmoja anadhurika na mmoja analipwa. Ndiyo kusema
kuwa, katika tendo la utoaji mimba, mtu [binadamu] aliyemo katika tumbo la mama anauawa;
mama mwenyewe anayemtoa mtoto huyo kafara kwa mwuaji anadhurika na mwuaji halisi,
yaani daktari, nesi au mtu mwingine yeyote yule anapata malipo, ujira kwa kazi yake
ya kuua. Katika vitendo vya utoaji mimba, kwa hiyo, hakuna aliye salama. Mtoto anakufa.
Mama anadhurika kimwili na kisaikolojia. Daktari licha ya kupata ujira wake anadhurika
kisaikolojia.
Kwa vile, vitendo vya utoaji mimba vinaelekezwa kwa binadamu,
aliye mdogo sana na asiyeweza kujitetea, na kwa vile utoaji mimba huhusisha umwagikaji
wa damu nyingi, na kwa vile vitendo hivyo vinafanywa na binadamu walio na nguvu kuelekea
kwa binadamu dhaifu, basi, vitendo vyote vya utoaji mimba ni vya kikatili, vya kimabavu
tena vyenye kumwaga damu nyingi na vya kinyama.
Katika hali ya kawaida akili
ya ya binadamu inaelekezwa katika kuhifadhi uhai wa mwingine, na si kuundoa. Ndiyo
sheria za nchi humwadhibu vikali mtu anayemwua mwingine, kwa kifungo cha maisha
na pengine kunyongwa. Kama hiyo ndiyo adhabu apataye mtu anayemwua mwingine, basi
kila mtoaji mimba anastahili adhabu hiyo.
Watetezi wa kifo wanatumia pia dhana
ya utoaji mimba salama, wakimaanisha utoaji mimba holela unaofanywa bila utaalamu
na katika mazingira hatarishi. Katika baadhi ya nchi matangazo huandikwa yenye ujumbe
“hapa utapata huduma ya utoaji mimba iliyo salama, isiyokuwa na maumivu, inayochukua
muda mfupi na ya gharama nafuu”.
Hoja zitolewazo kuwa utoaji mimba wa aina
hiyo ni kuwa hausababishi maumivu na vifo kwa akina mama. Lakini takwimu kutoka nchi
zile zilizoruhusu utoaji mimba kiusalama, yaani kitaalamu zinaonyesha kuwa wanawake
wanaokufa kwa utoaji mimba salama ni wengi zaidi kuliko katika nchi ambazo sheria
zake zinazuia kabisa utoaji mimba, na ambako ndiko wanadai kuna utoaji mimba usio
salama.
Vilevile tukumbuke kuwa siyo kwamba wanawake wakiruhusiwa kuua watoto
wao kiusalama, basi hawatakufa. Wanawake watoao mimba kiusalama watakufa na wakati
huo huoa wale watoa mimba pasipo salama watakufa kwani siyo kila mwanamke mwuaji
atakuwa na uwezo wa fedha za kumwulia mtoto wake kiusalama. Kwa hivyo vifo vya wanawake
watoaji mimba vitaongezeka.
Isitoshe, upiganiaji utoaji mimba salama unapofanywa
na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, unakiuka lengo la uwepo wa kituo hicho.
Tulitegemea Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kingepigania kuunga mkono sheria
zinazolinda haki ya kuishi, kama ambavyo Katiba ya Jamhuri ya Mwungano wa Tanzania
[1977] inasema. Haki ya kuishi ni haki ya mwanzo na ya msingi kwa kila mtu [binadamu]
na ambamo haki nyingine zote husimama. Na hii ni haki ya kila mtu, yule ambaye amezaliwa
na yule ambaye hajazaliwa. Hakuna mwenye mamlaka wala uhalali wa kukiuka haki hiyo.
Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kinapotetea haki ya kutoa mimba kiusalama
kina maana kuwa mtu [mama] ana haki ya kuishi na mtu[mtoto] ndani ya tumbo la mwanamke
ana haki ya kuuawa ili mradi mauaji hayo yafanyike kiusalama, yaani mtu [mtoto] afe
na mtu [mama] apone. Kama hivyo ndivyo inavyomaanisha, basi Kituo cha Sheria na Haki
za Binadamu kitakuwa kinakiuka lengo msingi la uwepo wake, yaani kupiganiana haki
za kila mtu [binadamu].
Vitendo vya utoaji mimba ni viovu kwa asili na tabia
yake. Kukubali kuwa mtu mmoja anaweza kumwua mwingine, ili mtu huyo anayeua asidhurike
au kufa ni vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu vinavyopaswa kulaaniwa na kila
mtetezi wa haki za binadamu. Na kwa tabia ya uovu, ukisharuhusu uovu mmoja, basi utazaa
uovu mwingine na hivyo kuyafanya mauaji ya watu wasioweza kujitetea kuwa sehemu ya
utamaduni kengeushi wa binadamu.
Wanawake watakuwa wamefunguliwa milango ya
kuua watoto wao [mimba] hata kwa visingizio vidogo tu, kama vile afya mama, uhai wa
mama, ulemavu wa mimba, mimba za ndugu hata mimba za ubakaji. Katika undani wake vitendo
hivyo vitabadilisha misingi ya maadili iliyolinda jamii kwa miaka mingi ya kulinda
na kutetea uhai wa binadamu, sasa tutageuza vitendo vya mauaji ya watoto kama tiba
kwa akina mama wajawazito.
Itakuwa kama hivi, “kwa kuogopa vitendo vya kutoa
mimba visivyo salama, dawa yake ni kuruhusu utoaji mimba ulio salama; kwa kuhofia
mimba zinazohatarisha afya ya mama au uhai wa mama, tiba yake ni kuua hiyo mimba ili
mama apone; kwa ulemavu wa mimba, mimba za ndugu na mimba za ubakaji, tiba yake ni
kuziua hizo mimba ili kukwepa aibu katika familia.
Hatudhani kwamba hilo ni
suluhisho la kweli. Suluhisho la kweli ni kuwatia hatiani wauaji wote. Daktari atumie
utaalamu na karama yake kumhudumia mama mgonjwa ili hali ni mja mzito au mama atishiwaye
na kifo kutokana na mimba aliyonayo. Daktari akiamua kumwua mtoto ili mama yake apone
atakuwa amekiuka misingi ya maadili ya tiba. Hapa nchini kuna sheria itokanayo na
makosa ya ubakaji na hata mimba za ndugu. Tunakishauri Kituo cha Sheria na Haki za
Binadamu kuhimiza utekelezwaji wa sheria hizo.