2013-08-05 07:55:45

Mchakato wa kuombea amani kutoka kwa Baraza la Maaskofu Katoliki Japan


Mama Kanisa anaendelea kuadhimisha Jubilee ya miaka 50 tangu Baba Mtakatifu Yohane wa Ishirini na tatu alipochapisha Waraka wa Amani Duniani, Pacem in Terris, ambao umekuwa ni Waraka rejea katika kujenga, kulinda na kutetea misingi ya haki, amani na upatanisho wa kweli miongoni mwa Jumuiya ya Kimataifa. RealAudioMP3

Ni waraka ambao ulitumwa kwa watu wote wenye mapenzi mema kunako tarehe 11 Aprili 1963, wakati ambapo dunia ilipokuwa inakabiliana na hali tete ya kuzuka kwa vita ya dunia. Hiki ni kipindi ambacho Ujerumani ilijikuta imegawanyika na Ukuta wa Berlin uliojengwa kunako mwaka 1961 ukawa ni kielelezo cha kinzani na mgawanyiko huu miongoni mwa wananchi wa Ujerumani.

Marekani na Urussi zilikuwa zinapimana nguvu na uwezo wa kivita ili kuoneshana ubabe, ambao ungeweza kugharimu maisha ya mamillioni ya watu! Cuba nikajikuta ikibanwa na mgogoro wa makombora, ulioibuka kunako mwaka 1962, hadi leo hii, Cuba inaendelea kugharimia mgogoro wa vita baridi na madhara yake yamekuwa ni makubwa kwa wananchi wa Cuba kwa kipindi cha miaka hamsini kwa kuwekewa vikwazo vya uchumi kimataifa! Kilele cha kinzani zote hizi za kivita ni pale ambapo Marekani na Urussi zilianza kutishia kutumia silaha za kinyuklia ili kukata mzizi wa fitina! Hapa maafa yangekuwa ni makubwa sana!

Wananchi wa Japani walionja madhara ya kinzani na Vita kuu ya Pili ya dunia, hadi leo hii bado kuna wananchi ambao wameathirika kutokana na mabomu ya Nyuklia yaliyorushwa nchini Japan. Kwa kutambua madhara ya vita, Baraza la Maaskofu Katoliki Japan, limeandaa siku kumi kwa ajili ya kuombea amani, kuanzia tarehe 6 hadi tarehe 15 Agosti, 2013.

Askofu mkuu Peter Takeo Okada wa Jimbo kuu la Tokyo, Japan, ambaye pia ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Japan katika ujumbe wake kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku kumi za Amani nchini Japan anasema kwamba, Waraka wa Amani Duniani unatoa mafundisho ya kina juhusu haki msingi za binadamu na wajibu wa kila mtu katika Jamii; Serikali na umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea mafao ya wengi. Unagusa masuala nyeti ya kimataifa kama vile: ukweli, haki, mshikamano, wakimbizi, rufuku ya matumizi ya silaha za kinyuklia pamoja na sera na mikakati ya maendeleo endelevu yanayomgusa mtu mzima: kiroho na kimwili.

Waraka huu unapania pamoja na mambo mengine kujenga msingi wa amani unaopata chimbuko lake katika ukweli, haki, upendo na uhuru; mambo nyeti katika kulinda na kudumisha utu, heshima na haki msingi za binadamu. Waraka huu unabainisha kwamba, maendeleo ya kweli ya mwanadamu yanaweza kupatikana ikiwa kama watu wanaishi katika amani, uelewano na mshikamano. Huu ni ujumbe endelevu hata katika ulimwengu mamboleo, ambamo, amani, utu na heshima ya binadamu vinaendelea kukabiliana na changamoto kubwa.

Tafakari ya kina juu ya Waraka wa Amani Duniani, sanjari na Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka Hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican, katika Mwaka wa Imani, ni fursa makini kwa waamini kutafakari tena tunu hizi msingi katika maisha na vipaumbele vyao. Kwa wananchi wa Japan, kuna maana ya pekee, wakati huu wanapofanya mchakato wa kutaka kubadilisha Katiba ya Nchi ambayo kimsingi ni sheria mama!

Askofu mkuu Peter Takeo Okada, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Japan anasema, mabadiliko ya Katiba yanataka kuondoa vifungu muhimu sana vinavyoonesha heshima na hadhi ya binadamu mintarafu mafundisho ya Kristo juu ya upendo na umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea: maisha, utu na heshima ya binadamu.

Tarehe 28 Aprili 2013 Japan iliadhimisha Kumbu kumbu ya Mkataba wa San Francisco, siku ile Japan ilipopewa heshima yake kama Taifa, ingawa kuna baadhi ya wananchi wa Japan hawakutendewa haki. Tarehe 23 Juni 2013, Japan iliwakumbuka wote waliopoteza maisha yao wakati wa vita. Matukio yote haya wanasema Maaskofu Katoliki Japan yawasidie waamini kutafakari kuhusu sera makini za kisiasa zinazoweza kujenga na kudumisha misingi ya haki na amani.








All the contents on this site are copyrighted ©.