2013-08-03 11:19:42

Vijana Karibuni Jimbo kuu la Cracovia, 2016


Kardinali Stanislaw Dziwisz, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Cracovia, mwenyeji wa Maadhimisho ya Siku ya 29 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016 amezindua mtandao kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016 kwa lugha ya Kiingereza. Unaweza kuperuzi kwenye mtandao huo kwa anuani ifuatayo: www.krakow2016.com.

Maadhimisho haya yatakuwa ni nafasi ya pekee kwa vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia kwa ajili ya kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa matendo makuu aliyolikirimia Kanisa lake kwa njia ya maisha na utume wa Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili, aliyewapenda vijana upeo na wakamwonesha kwamba, kwa hakika walikuwa wamemkubali, kiasi hata cha kupiga ukelele atangazwe kuwa mtakatifu mara moja!

Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili ni urithi mkubwa katika maisha na utume Kanisa. Ni kiongozi aliyeonesha utakatifu wa maisha na akawa ni mfano wa kuigwa miongoni mwa vijana kiasi cha kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani, huku wakiendeleza na kudumisha Ibada kwa Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa.

Kardinali Stanislaw anasema, Jimbo la Cracovia, kumekucha! Tayari waamini na wananchi wenye mapenzi mema, wameanza kujiandaa kwa ajili ya kuwapokea, kuwakaribisha na kuwakirimia vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Anasema, wanajiandaa kujitosa kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya vijana duniani, katika hali ya upendo, ukarimu, udugu na mshikamano wa upendo, ili kuwajengea vijana matumaini ya leo na kesho iliyo bora zaidi.









All the contents on this site are copyrighted ©.