Kanisa Katoliki Japan linawakumbuka wahanga wa Vita kuu ya Pili ya Dunia
Kardinali Peter Turkson, Rais wa Baraza la Kipapa la haki na amani, kuanzia tarehe
5 hadi tarehe 9 Agosti 2013 atakuwa na ziara ya kichungaji nchini Japan, ili kusali
na kutafakari pamoja na Kanisa Katoliki nchini Japan wanapowakumbuka wahanga wa mashambulizi
ya kinyuklia yalitokea Hiroshima na Nagasaki, wakati wa vita kuu ya pili ya dunia
kunako mwaka 1945.
Hija hii ya kichungaji inakwenda sanjari na Maadhimisho
ya Siku Kumi za Amani zilizotangazwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Japan, kuanzia
tarehe 6 hadi tarehe 15 Agosti 2013 kama njia ya kuwakumbuka waliopoteza maisha na
kuathirika katika mashambulizi ya mabomu ya Atomiki nchini Japan, ambako hata leo
hii, madhara yake bado yanaonekana.
Akiwa nchini Japan, Kardinali Turkson atashiriki
katika Ibada ya Misa takatifu; Majadiliano ya kidini na waamini wa dini kuu nchini
Japan kwa kuonesha umuhimu wa kushirikiana kama njia ya kusimama kidete kulinda na
kudumisha misingi ya haki na amani duniani.
Kardinali Turkson anatarajiwa kushiriki
katika majadiliano ya amani yaliyoandaliwa na Kituo cha Majadiliano ya Kidini mjini
Nagasaki na baadaye atashiriki pia katika Maadhimisho ya Mji wa Nagasaki kwa ajili
ya kuwakumbuka waathirika wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia nchini Japan, tukio linalotarajiwa
kuwashirikisha waamini kutoka katika dini mbali mbali nchini Japan.
Kardinali
Turkson, akiwa mjini Nagasaki, tarehe 9 Agosti 2013, atashiriki katika Ibada ya Misa
Takatifu kwa ajili ya kuombea amani duniani. Itakumbukwa kwamba, kunako mwaka 1981,
Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipotembelea Hiroshima, alikemea vita na kutaka amani
iweze kutawala katika maisha na mioyo ya watu duniani.
Papa Yohane Paulo wa
Pili, wakati huo, aliwataka viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kusimama kidete kupinga
vita kwani vita haijawahi kutatua matatizo na changamoto zinazowakabili watu wa mataifa
na badala yake, imekuwa ni chanzo cha taabu na mahangaiko ya watu wengi wasiokuwa
na hatia. Vijana wanachangamotishwa kwa namna ya pekee, kuhakikisha kwamba, wanakataa
na kupinga matumizi ya vita, kwani mara nyingi wao ndio wanaokuwa wa kwanza kupelekwa
mstari wa mbele.
Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili anawaalika vijana kujenga
na kuimarisha mshikamano wa upendo na udugu, kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya binadamu
wote. Tangu wakati huo, Baraza la Maaskofu Katoliki Japan, limeendelea kuhamasisha
Jamii kujikita katika misingi ya haki na amani, daima wakitambua kwamba, amani na
utulivu ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu, inayowashirikisha binadamu, lakini kwa
namna ya pekee viongozi wa nchi kwani wao wanachukua dhamana na maamuzi makubwa kwa
ajili ya wananchi wao.
Jamii ya Kimataifa inahamasishwa kuwa ni wajenzi na
vyombo vya amani kwa kuachana na dhana ya vita ambayo kimsingi inaendelea kusababisha
maafa makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia. Baraza la Maaskofu Katoliki Japan linaendelea
kuadhimisha Jubilee ya Miaka 50 tangu Mwenyeheri Yohane wa XXIII alipochapisha Waraka
wa kichungaji, Pacem in Terris, Amani Duniani. Ni Waraka unaofafanua dhamana na haki
ya kila mtu; jukumu la Serikali katika kutafuta na kuendeleza mafao ya wengi.
Ni
Waraka unaopembua kwa kina na mapana kuhusu: ukweli, haki, mshikamano, tatizo la wakimbizi,
mchakato wa kudhibiti biashara ya silaha duniani; uchumi na maendeleo endelevu yanayogusa
mahitaji msingi ya binadamu kiroho na kimwili. Amani ni fadhila kwa ajili ya binadamu
wote inayopaswa kujikita katika ukweli, upendo na uhuru. Ili kudumisha amani, kuna
haja ya kusimama kidete kulinda na kutetea haki msingi za binadamu na kwamba, amani
ni kikolezo kikubwa cha maendeleo endelevu kinachopania kujenga na kuimarisha Jamii
inayojipambanua katika misingi ya kiutu!