Tafakari ya Neno la Mungu Jumapili ya 18 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa
Mpendwa mwana wa Mungu karibuni tena katika kipindi cha tafakari ya Neno la Mungu,
ili tushirikishane upendo wa Mwenyezi Mungu kwa njia ya Neno lake lililo hai.
Tayari ni
Dominika ya 18 ya mwaka C. Mama Kanisa ametuandalia meza ya Neno inayotupeleka kutambua
kuwa yafaa kuwa na Hekima katika kutafuta mali na kuwa na mali hizo. Bwana, katika
somo la Injili anakuja na neno kali dhidi ya tajiri anayeona aweza kuzuia kifo kwa
njia ya mali.
Bwana anasema mpumbavu we! Mhubiri katika somo la kwanza anasema
ni ubatili mtupu na Mtakatifu Paulo katika somo la Pili anataka mmoja akishafufuliwa
pamoja na Kristo kwa njia ya ubatizo basi daima ayatazame mambo ya juu, yaani kuyacha
yale yanayopingana na upendo wa kweli.
Mpendwa msikilizaji, kwa nini huyu ndugu
tajiri katika Injili anaonekana kujiweka katika mazingira ya kuridhika na mali akitafuta
kujifurahisha na kujiridhisha? Kipi kinampeleka mpaka hapo? Injili haituambii moja
kwa moja juu ya kuwa navyo na kuvifurahia! Lakini hebu tuangalie, Bwana anasema mpumbavu
we! Usiku huu roho yako itachukuliwa!
Basi maneno ya Bwana yaweza kutusaidia
kuelewa kuwa huyu Bwana alikuwa na hofu ya kifo kumbe sasa anaona angalau ajishibishe
kwa mali yake akidhani aweza hata kuzuia kifo. Haya ndiyo mawazo yaliyo ya wengi na
hasa wazee katika ulimwengu huu. Badala ya kufikiri mambo ya uzima wa milele huanza
kufikiria juu ya vitu, nitaviacha namna gani! Mshikamano na vitu hukua na kuongezeka!
Bwana anasema mpumbavu we! Leo usiku wanahitaji roho yako.
Mpendwa mwana wa
Mungu tuombe kuepukana na tatizo hili la mali. Mali iwe kwa ajili ya mafaa ya wokovu
na si kwa mafaa ya kujishibisha na kujenga mshikamano unaoondoa maisha ya mapendo
kwa wengine. Tabia hii si ngeni sana katika historia, nakumbuka katika historia ya
falsafa, Warumi walikuwa wakisistiza juu ya suala hilo la kujiridhisha na kujifurahisha
kwa chakula, kwa sababu ya maisha kuwa mafupi!
Mpendwa maisha yetu ni zawadi,
ufupi na urefu si hoja, hoja ni kuishi katika kutimiza mapenzi ya Mungu. Waangalie
watakatifu vijana: Dominico Saverio, Gabriele wa Shirika la Wamissionari wa Mateso,
Gema Galgani, Theresia wa Mtoto Yesu na wengineo katika ujana yaani ufupi wa miaka
yao wamefanya maajabu zawadi za kimungu kwetu.
Mpendwa mwana wa Mungu, Injili
inataka kutufundisha utajiri usioogopa kifo, bali utajiri unaoambatana na mapendo
makamilifu ya Mwenyezi Mungu. Utajiri unaojikita katika hekima ya kimungu, unaotambua
siri ya maisha, unaotambua jumuiya na maisha ya pamoja kinyume na uchoyo anaouonesha
tajiri huyu katika Injili.
Injili yataka kadri tunavyosonga mbele katika maisha
yetu tunapaswa kukua katika kujitenga na msongo wa mali ili muunganiko na Bwana ukue
siku kwa siku na hata siku moja tufurahi pamoja na Kristo mfufuka huko mbinguni. Huu
ndio utajiri wa kweli ndiyo maana ya ubatizo wetu.
Nikutakie hekima na heri
tele za Bwana siku kwa siku katika maisha yako. Tumsifu Yesu Kristo.
Tafakari
hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.