Baba Mtakatifu Francisko alipokuwa anarejea kutoka katika hija yake ya kichungaji
nchini Brazil kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani alimshukuru
Mungu kwa kufanikisha sherehe hii kubwa ya imani ambayo imeushirikisha umati mkubwa
wa waamini na watu wenye mapenzi mema kutoka sehemu mbali mbali za dunia.
Askofu
mkuu Oran Joao Tempesta wa Jimbo kuu la Rio de Janeiro akizungumza na waandishi wa
habarimapema juma hili, anasema kwamba, Kanisa linamshukuru Mwenyezi Mungu kwa mafanikio
makubwa yaliyopatikana katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013
huko Rio de Janeiro. Anasema hata Baba Mtakatifu Francisko anakiri kwamba, Rio kwa
Mwaka 2013 imefunika na kwamba, Kanisa limewahudumia vyema vijana waliohudhuria.
Askofu
mkuu Tempesta anasema, ufuko wa Copacabana haujawahi kufurika na watu kiasi hiki,
wote hawa wakiwa na amani na utulivu wa ndani, huku wakipania kusikiliza ujumbe uliokuwa
unatolewa na Khalifa wa Mtakatifu Petro; wengi wameguswa na wanataka kuona matunda
ya Maadhimisho haya yanaleta mabadiliko ili dunia iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi
pa kuishi.
Ni matumaini ya Mama Kanisa kwamba, vijana wa kizazi kipya wataendelea
kuwa ni wajenzi wa misingi ya haki, amani na upatanisho miongoni mwa Jamii zao, tayari
kujitosa kimaso maso kwa ajili ya kutangaza Injili ya Kristo hadi miisho ya dunia.
Askofu
mkuu Tempesta anasema kwamba, zaidi ya watu millioni 3.5 wameshiriki katika Maadhimisho
ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013. Maadhimisho haya yamefanyika kwenye
ufuko wa Copacabana, Quinta da Boa na viunga vya Mji wa Rio. Brazil, Argentina, Marekani,
Chile, Italia, Venezuela, Ufaransa, Paraguay, PerĂ¹ na Mexico ni nchi ambazo zilikuwa
na wawakilishi wengi zaidi. Bara la Afrika pia liliwakilishwa barabara na makundi
makubwa ya vijana; VIjana wa Afrika hawakuvuma, lakini wamo!
Takwimu zinaonesha
kwamba, asilia 55% ya mahujaji waliohudhuria walikuwa ni wanawake na wasichana, wakati
wanaume na vijana walikuwa ni asilimia 45%. Ndiyo maana hata Baba Mtakatifu Francisko
wakati wa mazungumzo yake na Waandishi wa habari waliokuwa kwenye msafara wake kwenye
hija yake ya kichungaji nchini Brazil alisema kwamba, wanawake wanapaswa kupewa nafasi
kubwa zaidi katika kushiriki maisha na utume wa Kanisa, hasa wakati huu wa Uinjilishaji
mpya.
Idadi ya mahujaji waliojiandikisha kushiriki katika Maadhimisho ya Siku
ya 28 Vijana Duniani inaonesha kwamba, asilimia 60% ya watu wote walikuwa ni vijana
wenye umri kati ya miaka 19 hadi 34. Vijana waliojitolea kuwahudumia vijana wenzao
kutoka sehemu mbali mbali za dunia walikuwa ni 60,000. Waandishi wa habari waliohakikisha
kwamba, watu wanapata kwa wakati muafaka yale yaliyokuwa yanajiri huko Rio walikuwa
ni 6,500 kutoka katika nchi 57.
Jimbo kuu la Rio de Janeiro liliandaa vituo
264 vya Katekesi iliyotolewa katika lugha 25 za Kimataifa. Kulikuwa na masanduku 1000
yaliyotumiwa kwa ajili ya Sakramenti ya Upatanisho. Maaskofu waliohudhuria walikuwa
ni 644 na kati yao kulikuwa na Makardinali 28. Mapadre walikuwa ni 7, 814 na Idadi
ya Mashemasi ilikuwa ni 632. Takwimu za uchumi zilizotolewa na Wizara ya Utalii zinaonesha
kwamba, watu wametumia kiasi cha dolla za kimarekani millioni 780 wakati walipokuwepo
nchini Brazil.