2013-08-02 07:54:53

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania na mafanikio ya Benki ya Mkombozi


Benki ya Mkombozi ambayo ni tunda na juhudi za Kanisa Katoliki katika kumkomboa mtanzania wa kawaida kwa kumjengea uwezo wa kiuchumi inaendelea vyema. Kwa kipindi cha miaka mitatu na nusu tangu ifunguliwe imekwisha fungua matawi manne. RealAudioMP3

Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linamshukuru Mwenyezi Mungu kwa mafanikio yote yaliyokwisha kupatikana katika kipindi.

Maaskofu wanawaomba wale walionunua hisa zao kwenye Benki ya Mkombozi kuvuta subira, kwani mchakato wa kufungua matawi mapya umekwamisha kidogo zoezi la kuanza kugawana faida. Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania linasema, kuwa na matawi mapya ni faida, kwani Benki ya Mkombozi itaweza kutoa huduma kwa watu wengi zaidi. Lengo la Benki hii ni kuhakikisha kwamba, inafika Tanzania nzima kwa haraka iwezekanavyo!

Hii ni sehemu ya barua iliyoandikwa na Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania akiwataka waamini na wote walionunua hisa katika Benki ya Mkombozi, kujifunga kibwebwe ili kuweza kukabiliana na changamoto iliyotolewa hivi karibuni na Benki kuu ya Tanzania kwa kuagiza kwamba, Mabenki yote nchini kuongeza hisa zake kutoka Billioni tano, Kiwango cha sasa hadi kufikia Billioni kumi na tano.

Baraza la Maaskofu linawaomba waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuona kwamba, Benki ya Mkombozi ni chombo makini cha kuwalatea watanzania maendeleo endelevu na kwamba, wanapaswa kuonesha uzalendo kwa kuchangia kwa hali na mali katika harakati za kufanikisha ongezeko la mtaji. Jambo hili linawezekana kwa kununua tena hisa kutoka katika Benki ya Mkombozi, kwa mtaji mkubwa zaidi, pengine kuliko ilivyokuwa hapo awali.

Mama Edwina Lupembe, Mkurugenzi mtendaji wa Benki ya Mkombozi ameanza zoezi ka kuhamasisha upatikanaji wa mtaji huu kutoka sehemu mbali mbali za Tanzania. Baraza la Maaskofu Katoliki linawaalika waamini na watu wenye mapenzi mema kuonesha moyo wa ushirikiano, ili kufanikisha zoezi hili.

Wadau wajijengee utamaduni na mazoea ya kutumia huduma mbali mbali zinazotolewa na Benki ya Mkombozi: kwa kuweka na kukopa pamoja na kuwaalika marafiki, ndugu na jamaa kujiunga na Benki ya Mkombozi.

Itakumbukwa kwamba, Benki ya Mkombozi inatoa pia huduma za fedha za kigeni, kumbe watu wanaweza kuitumia kwa kuzingatia maelezo ya utumaji wa fedha za kigeni kwa kupitia Benki ya Mkombozi.








All the contents on this site are copyrighted ©.