Queen Said ni Mratibu wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio nchini Tanzania katika mahojiano
maalum na Radio Vatican anabainisha kwamba, vijana wa kizazi kipya kwa sasa wamemezwa
mno na malimwengu, wanajitafuta wao wenyewe na hata wakati mwingine, wanashindwa kuguswa
na shida pamoja na mahangaiko ya watu wanaowazunguka.
Hawa ni wazee,
watoto yatima na wale wanaoishi katika mazingira hatarishi, maskini na wote wanaosukumizwa
pembezoni mwa jamii, wale ambao jamii inawataza kwa jicho la kengeza!
Vijana
wanapaswa kutambua umuhimu wa kujihusisha na matatizo na mahangaiko ya jirani zao,
vinginevyo, Jamii itakuwa inaunda vijana wa kizazi kisichojali wala kuguswa na matatizo
ya wengine, jambo ambalo ni hatari kabisa kwa sasa na kwa siku za usoni. Vijana wengi
wamegubikwa na uchu wa mali, fedha, sifa na tamaa za ujana kiasi kwamba, sasa imekuwa
ni nongwa au kwa maneno ya vijana wenyewe imekuwa ni "noma".
Queen Said anasema,
Baba Mtakatifu Francisko anawachangamotisha waamini lakini zaidi vijana kujenga na
kuimarisha utamaduni wa kujali na kuguswa na mateso pamoja na mahangaiko ya jirani
zao, ili kujenga na kudumisha utamaduni wa upendo na mshikamano wa dhati.
Vijana
wajifunze kujitosa kimasomaso bila hata ya kujibakiza chembe kwa ajili ya Mungu na
jirani zao; vijana waonje na kuguswa na umaskini wa ndugu zao katika Kristo, kama
anavyoendelea kukazia Baba Mtakatifu Francisko. Vijana wanachangamotishwa kumwilisha
yale waliyojifunza kutoka katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka
2013, kwa kukumbatia mafundisho ya Kristo na changamoto zake, ili kwenda ulimwenguni
kote kuwafanya mataifa kuwa ni wanafunzi wa Yesu.
Queen Said anasema ni mwaliko
na changamoto kwa vijana kurudi ndani ya Kanisa ili kumjifunza tena Yesu Kristo, kwa
kumwilisha mafundisho na vipaumbele vyake katika ujenzi wa Ufalme wa Mungu hadi miisho
ya dunia. Nchini Tanzania, Jumuiya ya Mtakatifu Egidio inatekeleza utume wake miongoni
mwa watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira hatarishi kule Mwenge, Jimbo kuu la
Dar es Salaam, Kituo cha Wazee Funga funga kilichoko Jimbo Katoliki Morogoro; inawahudumia
pia watoto waliofungwa kwenye gereza la watoto watukutu, Manispaa ya Mbeya.
Queen
Said anabainisha kwamba, vijana ni chachu ya maendeleo, mabadiliko na furaha katika
Jamii, wakitaka wanaweza kumwilisha tunu hizi katika uhalisia wa maisha, changamoto
kwa kila kijana kujitoa kwa ajili ya wengine, ili kujenga na kudumisha dunia ambayo
ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.