2013-08-01 11:41:57

Upendo na uaminifu hukutana pamoja, haki na amani hubusiana!


Jumuiya ya Mtakatifu Agidio yenye makao yake makuu mjini Roma ni familia kubwa ya waamini walei kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanaoendelea kujitosa kimasomaso kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao na kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu.

Kuanzia tarehe 2 hadi tarehe 4 Agosti 2013, wawakilishi wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio nchini Tanzania wanakutana Jimbo kuu la Arusha, kama njia ya kuwakumbuka wale waliopoteza maisha yao na wengine wengi kujeruhiwa wakati bomu liliporushwa kwenye Parokia ya Mtakatifu Olasti ya Mtakatifu Yosefu, Mfanyakazi, Jimbo kuu la Arusha hivi karibuni.

Mkutano huu unaongozwa na kauli mbiu "Upendo na uaminifu hukutana pamoja, haki na amani hubusiana" Zaburi ya 85. Wanajumuiya wanapenda kuanza mkutano wao kwa kuwakumbuka waathirika wa mabomu Jimbo kuu la Arusha, kama mwaliko wa kusimama kidete kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na upatanisho miongoni mwa Jamii.

Wanachama wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio wanashiriki katika utekelezaji wa malengo na mikakati ya Jumuiya hii kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa sala, uenezaji wa Habari Njema ya Wokovu, kama sehemu ya utekelezaji wa maisha yao kama wabatizwa. Ni watu wanaohamasishwa kujenga na kudumisha mshikamano wa dhati na maskini pamoja na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali na nafasi yao katika Jamii husika.

Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican wanaendelea kukazia umuhimu wa kuyatakatifuza malimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha unaojikita katika majadiliano ya kidini na kiekumene, kama njia ya kuhamasisha mchakato wa ujenzi wa misingi ya haki, amani na upatanisho miongoni mwa Jamii.









All the contents on this site are copyrighted ©.