Tanzania na Thailand watiliana sahihi mkataba wa ushirikiano na uhusiano!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete na Waziri Mkuu wa
Thailand, Yingluck Shinawatra Jumanne, Julai 30, 2013 wameshuhudia utiaji saini mikataba
minne ya kuimarisha ushirikiano na uhusiano kati ya nchi hizo mbili. Viongozi hao
wawili wameshuhudia utiaji saini huo katika shughuli fupi iliyofanyika Ikulu, Dar
es Salaam mchana ikiwa sehemu ya shughuli za Mheshimiwa Shinawatra katika Tanzania
wakati wa ziara yake ya siku tatu nchini.
Mikataba ambayo viongozi hao wameshuhudiwa
ikitiwa saini ni pamoja na ule wa kubadilisha wafungwa uliotiwa na Naibu Waziri wa
Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Silima Pereira kwa niaba ya Tanzania na Naibu Waziri
Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Thailand, Mheshimiwa Surapong Tovichachakul. Mikataba
mingine ni mkataba wa Kuimarisha na Kulinda Uwekezaji (Promotion and Protection of
Investments) na mkabata wa Ushirikiano katika Masuala ya Ufundi iliyotiwa saini na
Mheshimiwa Tovichachakul na Waziri wa Fedha wa Tanzania, Mheshimiwa William Mgimwa.
Mkataba
wa nne kutiwa saini ni Makubaliano kati ya Wizara ya Nishati na Madini na Chuo cha
Madini cha Thailand kwa niaba ya Wizara ya Biashara ya Thailand uliotiwa saini na
Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Bwana Eliakim Maswi na Mkurugenzi Mkuu wa Chuo cha
Madini cha Thailand Bi. Prom Sawatwatthanakul.
Mapema siku ya Jumanne, Waziri
Mkuu wa Thailand ambaye aliwasli nchini akitokea Msumbiji katika ziara yake ya nchi
tatu za Afrika amepokelewa kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA)
na pia akalakiwa Ikulu, Dar Es Salaam na mwenyeji wake Rais Kikwete.
Viongozi
hao wamekutana na kufanya mazungumzo ya faragha na baadaye kufanya mazungumzo rasmi
ya Kiserikali kati ya Serikali hizo mbili. Kubwa ambalo limekubaliwa katika mazungumzo
hayo ni umuhimu wa nchi hizi mbili kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati yao kwa
manufaa ya wananchi wa Tanzania na Thailand.
Baadaye viongozi hao wawili wamekwenda
kwenye Hoteli ya Hyatt Regency-Kilimanjaro mjini Dar Es Salaam ambako Mheshimiwa Shinawatra
ametangaza Mpango Mpya wa Ushirikiano kati ya Afrika na Thailand.
Mama huyo
ameuambia mkutano huo wa maofisa wa Serikali, wafanyabiashara wa sekta binafsi, wasomi,
mabalozi na wanadiplomasia pamoja na wawakilishi wa taasisi zisizokuwa za Kiserikali
kuwa Mpango huo una misingi yake katika ushirikiano wa Nchi Zinazoendelea za Kusini
(South-South Cooperation).
Chini ya Mpango huo, Thailand itaitisha mkutano
wa kwanza wa wakuu wa nchi za Afrika na Thailand mwanzoni mwa mwaka ujao na amemwalika
Rais Kikwete kuhudhuria mkutano huo wenye nia ya kujenga mahusiano ya karibu zaidi
kati ya Afrika na Thailand. “Kwa kutilia maanani usawa wa ujuzi wa jitihada za maendeleo
nchi za Afrika na Thailand, nchi yangu itaongeza kasi ya mahusiano ya maendeleo na
Afrika katika maeneo ambako uhusiano huo unaweza kuongeza faida kwa pande zote mbili,
kwa jamii zetu na watu wetu hasa katika sekta za kilimo, afya, elimu na maendeleo
ya watu kwa jumla.”
Ameongeza Mama huyo: “Wakati huo huo, Thailand inatangaza
leo kuanzishwa kwa Mpango wa Wanathailand Kujitolea ambako wataalam wa Thailand watafanya
kazi na wenzao wa Afrika katika nchi za Afrika kwenye miradi iliyoko chini ya ushirikiano
wa kiufundi.”
Baadaye, Waziri Mkuu Shinawatra amehudhuria dhifa ya kitaifa
ambayo iliandaliwa kwa heshima yake na Rais Kikwete, Ikulu, Dar Es Salaam.
Jumatano,
Waziri Mkuu huyo atakwenda kwenye Mbunga ya Taifa ya Serengeti ambako atakutana na
maofisa wa Wizara ya Maliasili na Utalii watakaomwelezea hali halisi, changamoto na
umuhimu wa kulinda mbunga za wanyama. Aidha, akiwa Serengeti, mama huyo atashuhudia
utiaji saini wa Makubaliano ya Kushirikiana Katika Kulinda Hifadhi na Wanyamapori
kati ya Serikali za Tanzania na Thailand, ikiwa ni pamoja na kushirikiana katika kupambana
dhidi ya ujangili.