2013-07-31 09:04:21

Tanzania na Thailand watiliana sahihi mkataba wa ushirikiano na uhusiano!


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete na Waziri Mkuu wa Thailand, Yingluck Shinawatra Jumanne, Julai 30, 2013 wameshuhudia utiaji saini mikataba minne ya kuimarisha ushirikiano na uhusiano kati ya nchi hizo mbili. Viongozi hao wawili wameshuhudia utiaji saini huo katika shughuli fupi iliyofanyika Ikulu, Dar es Salaam mchana ikiwa sehemu ya shughuli za Mheshimiwa Shinawatra katika Tanzania wakati wa ziara yake ya siku tatu nchini.

Mikataba ambayo viongozi hao wameshuhudiwa ikitiwa saini ni pamoja na ule wa kubadilisha wafungwa uliotiwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Silima Pereira kwa niaba ya Tanzania na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Mambo ya Nje wa Thailand, Mheshimiwa Surapong Tovichachakul. Mikataba mingine ni mkataba wa Kuimarisha na Kulinda Uwekezaji (Promotion and Protection of Investments) na mkabata wa Ushirikiano katika Masuala ya Ufundi iliyotiwa saini na Mheshimiwa Tovichachakul na Waziri wa Fedha wa Tanzania, Mheshimiwa William Mgimwa.

Mkataba wa nne kutiwa saini ni Makubaliano kati ya Wizara ya Nishati na Madini na Chuo cha Madini cha Thailand kwa niaba ya Wizara ya Biashara ya Thailand uliotiwa saini na Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini Bwana Eliakim Maswi na Mkurugenzi Mkuu wa Chuo cha Madini cha Thailand Bi. Prom Sawatwatthanakul.

Mapema siku ya Jumanne, Waziri Mkuu wa Thailand ambaye aliwasli nchini akitokea Msumbiji katika ziara yake ya nchi tatu za Afrika amepokelewa kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) na pia akalakiwa Ikulu, Dar Es Salaam na mwenyeji wake Rais Kikwete.

Viongozi hao wamekutana na kufanya mazungumzo ya faragha na baadaye kufanya mazungumzo rasmi ya Kiserikali kati ya Serikali hizo mbili. Kubwa ambalo limekubaliwa katika mazungumzo hayo ni umuhimu wa nchi hizi mbili kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati yao kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na Thailand.

Baadaye viongozi hao wawili wamekwenda kwenye Hoteli ya Hyatt Regency-Kilimanjaro mjini Dar Es Salaam ambako Mheshimiwa Shinawatra ametangaza Mpango Mpya wa Ushirikiano kati ya Afrika na Thailand.

Mama huyo ameuambia mkutano huo wa maofisa wa Serikali, wafanyabiashara wa sekta binafsi, wasomi, mabalozi na wanadiplomasia pamoja na wawakilishi wa taasisi zisizokuwa za Kiserikali kuwa Mpango huo una misingi yake katika ushirikiano wa Nchi Zinazoendelea za Kusini (South-South Cooperation).

Chini ya Mpango huo, Thailand itaitisha mkutano wa kwanza wa wakuu wa nchi za Afrika na Thailand mwanzoni mwa mwaka ujao na amemwalika Rais Kikwete kuhudhuria mkutano huo wenye nia ya kujenga mahusiano ya karibu zaidi kati ya Afrika na Thailand. “Kwa kutilia maanani usawa wa ujuzi wa jitihada za maendeleo nchi za Afrika na Thailand, nchi yangu itaongeza kasi ya mahusiano ya maendeleo na Afrika katika maeneo ambako uhusiano huo unaweza kuongeza faida kwa pande zote mbili, kwa jamii zetu na watu wetu hasa katika sekta za kilimo, afya, elimu na maendeleo ya watu kwa jumla.”


Ameongeza Mama huyo: “Wakati huo huo, Thailand inatangaza leo kuanzishwa kwa Mpango wa Wanathailand Kujitolea ambako wataalam wa Thailand watafanya kazi na wenzao wa Afrika katika nchi za Afrika kwenye miradi iliyoko chini ya ushirikiano wa kiufundi.”

Baadaye, Waziri Mkuu Shinawatra amehudhuria dhifa ya kitaifa ambayo iliandaliwa kwa heshima yake na Rais Kikwete, Ikulu, Dar Es Salaam.

Jumatano, Waziri Mkuu huyo atakwenda kwenye Mbunga ya Taifa ya Serengeti ambako atakutana na maofisa wa Wizara ya Maliasili na Utalii watakaomwelezea hali halisi, changamoto na umuhimu wa kulinda mbunga za wanyama. Aidha, akiwa Serengeti, mama huyo atashuhudia utiaji saini wa Makubaliano ya Kushirikiana Katika Kulinda Hifadhi na Wanyamapori kati ya Serikali za Tanzania na Thailand, ikiwa ni pamoja na kushirikiana katika kupambana dhidi ya ujangili.








All the contents on this site are copyrighted ©.