2013-07-31 15:17:42

Kristo na Kanisa lake apewe kipaumbele cha kwanza na Wayesuit


Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Mtakatifu Inyasi wa Loyola, Mwanzilishi wa Shirika la Wayesuit, ameadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kanisa kuu la Gesù liloloko mjini Roma. Ibada hii imehudhuiriwa na Wayesuit, wafanyakazi na wadau mbali mbali katika maisha na utume wa Wayesuit mjini Roma.

Baba Mtakatifu katika mauhibiri yake amewataka Wayesuit na wadau wao kumweka Kristo kuwa ni kiini cha maisha na utume wao ndani ya Kanisa. Baba Mtakatifu pia amemkumbuka kwa namna ya pekee, Padre Paolo Dall'Oglio anayetekeleza utume wake nchini Syria, kwa sasa hajulikani mahali alipo. Wayesuit wanaalikwa kwa namna ya pekee kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu na jirani zao. Hivi ndivyo walivyofanya akina Mtakatifu Francisko Saverio na Padre Pedro Arupe, aliyekuwa mkuu wa Shirika la Wayesuit kwa miaka mingi.

Baada ya Ibada ya Misa Takatifu, Baba Mtakatifu amebaki na Wayesuit kwa takribani masaa mawili, akapata kifungua kichwa pamoja na kuzungumza nao. Kwa Wayesuit hii imekuwa ni siku maalum sana inayoacha chapa ya kudumu katika maisha na utume wao kwa Kristo na Kanisa lake.

Padre Adolfo Nicolas, Mkuu wa Wayesuit anasema, Baba Mtakatifu ndiye mkuu wala hana tena kifungo cha kuweka nadhiri ya nne ya utii kwa Baba Mtakatifu. Ni kiongozi huru kwa ajili ya huduma kwa Kanisa la Kristo na wala hakuna mkanganyo wa uwajibikaji katika masuala ya uongozi. Kwa njia hii, inakuwa ni rahisi kwa Wayesuit kujenga na kuimarisha umoja na Kanisa.

Baba Mtakatifu Francisko mara tu baada ya Ibada ya Misa takatifu amekwenda kutoa heshima yake kwenye Kaburi la Mtakatifu Inyasi, Mtakatifu Francisko Saverio na kaburi la Padre Pedro Arrupe, aliyekuwa ni kiongozi makini wa Wayesuit.







All the contents on this site are copyrighted ©.