2013-07-29 08:49:40

Poland inaanza kufungua malango yake kwa Maadhimisho ya Siku ya 29 ya Vijana Duniani kwa kumkumbuka Mwenyeheri Yohane Paulo II


Kardinali Stanislaw Dziwisz, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Cracovia, Poland anasema, amepokea kwa moyo mkuu ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko wa kuadhimisha Siku ya 29 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2016, Jimbo kuu la Cracovia, nchini Poland. Hii ni habari ya furaha, dhamana na uwajibikaji mkubwa mbele yao. Mwaka 2016, Poland itakuwa inaadhimisha miaka 1050 ya Uinjilishaji.

Kanisa na Serikali ya Poland, inamshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kupokea mwaliko kutoka Poland ulioonesha hamu na kiu ya vijana wengi kutaka kuadhimisha sherehe ya imani yao nchini Poland kwa kumkumbuka kwa namna ya pekee Mwenyeheri Yohane Paulo ambaye kunako mwaka 1978 aliondoka nchini Poland kwa kukabidhiwa dhamana ya kuwa ni Khalifa wa Mtakatifu Petro na muasisi wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani.

Daima Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alikuwa na matumaini makubwa kwa vijana katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Poland inaanza kufungua malango yake ili kwamba, katika kipindi cha miaka mitatu kuanzia sasa, iweze kuwapokea mahujaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Poland inamshukuru Baba Mtakatifu Francisko ambaye ameonesha nia ya kutaka kutembelea Poland, mahali alipozaliwa Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili ambaye anatarajiwa kutangazwa na Mama Kanisa kuwa Mtakatifu hivi karibuni.







All the contents on this site are copyrighted ©.