Brazil, Kwa herini! Tutaonana tena Mungu akipenda!
Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya kuhitimisha Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana
Duniani kwa Mwaka 2013 kwa Ibada ya Misa Takatifu kwenye ufuko wa Copacabana, Rio
de Janeiro, Brazil, tukio ambalo limehudhuriwa na watu millioni tatu, amewashukuru
na kuwaaga wananchi wa Brazil na kwa namna ya pekee, Rais Dilma Vana Rousseff kwa
niaba ya wananchi wa Brazil kwa matendo makubwa waliyomfanyia Khalifa wa Mtakatifu
Petro.
Baba Mtakatifu Francisko anasema, anarejea mjini Vatican akiwa amesheheni
matukio ya furaha ambayo kwa sasa yanageuka kuwa ni sala. Anasikia ile hamu ya kuendelea
kukaa na wananchi wa Brazil, waliomwonesha moyo wa ukarimu na urafiki. Anawashukuru
kwa tabasamu la nguvu na la kweli walilommegea wakati wote alipokuwa anakutana nao
bila kusahau sadaka na majitoleo ya vijana wengi walioacha shughuli zao ili kuweza
kuwakirimia upendo na huduma, ndugu zao katika Kristo.
Anawakumbuka vijana
aliokutana nao kwenye Hospitali ya Mtakatifu Francisko inayowahudumia waathirika wa
dawa za kulevya, bila kusahau upendo wa wananchi wa kitongoji cha Varginha. Baba Mtakatifu
anasema, kwa hakika anaona mkono wa Yesu ukitenda kazi miongoni mwa vijana na kwa
umati mkubwa wa watu aliokutana nao katika kipindi cha juma zima, muda ambao kamwe
hataweza kusahau katika maisha na utume wake!
Baba Mtakatifu anaendelea kuwashukuru
kwa namna ya pekee vijana waliokuwa ni kiini cha Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana
Duniani kwa Mwaka 2013. Wengi wao walikuja kama wafuasi wa Kristo, sasa wanarudi makwao
wakiwa wamefundwa na kuiva kama Wamissionari. Ni vijana ambao wako tayari kutolea
ushuhuda wa maisha yao kwa njia ya furaha, huduma, daima wakijitahidi kujenga utamaduni
wa upendo. Ni vyema vijana wakasimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya
binadamu sanjari na kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Injili ya Kristo.
Baba
Mtakatifu anawakumbusha vijana kwamba, Yesu ndiye aliyekuwa wa kwanza kuanza mchakato
wa kuwatafuta, anapenda kuwasha moto wa Injili ili waweze kwenda kutangaza Habari
Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia. Baba Mtakatifu anasema, yeye binafasi amekwisha
onja baadhi ya matunda ya kazi hii, wengine wataendelea kufurahia katika utimilifu
wake.
Baba Mtakatifu Francisko amemshukuru Bikira Maria wa Aparecida. Anasema,
kwenye madhabahu ya Bikira Maria wa Aparecida, amepiga magoti kwa ibada kwa ajili
ya kuombea dunia, lakini kwa namna ya pekee wananchi wa Brazil. Anasema, amemwomba
Bikira Maria ili aweze kuimarisha imani ya Kikristo nchini Brazil kama ilivyo hata
kwa nchi nyingine duniani; imani ambayo ni amana kubwa kwa utamaduni wa wananchi wa
Brazil.
Ni mwaliko anasema Baba Mtakatifu wa kuendelea kujenga na kudumisha
amani na mshikamano kati ya watu. Mwishoni kabisa, Baba Mtakatifu anaendelea kuwaomba
wananchi wa Brazil na wote wenye mapenzi mema kumsindikiza katika maisha na utume
wake kwa njia ya Sala, kwani anauhitaji mkubwa wa sala!