Vijana kutoka Bara la Afrika waguswa na ukarimu wa wananchi wa Brazil
Wawakilishi wa vijana kutoka Barani Afrika ni kati ya bahari ya watu ambao imekuwa
ikihudhuria Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 huko Rio de
Janeiro. Licha ya uchovu, mvua na pilika pilika za maadhimisho haya, vijana kutoka
Barani Afrika wanasema, wameonja umoja na mshikamano katika imani, matumaini na mapendo
kutoka kwa vijana wanaohudhuria Maadhimisho ya Siku ya Vijana huko Rio de Janeiro.
Kwa hakika, kimekuwa ni kipindi cha kujenga na kuimarisha Umoja na Mshikamano
kati ya Kanisa la kiulimwengu pamoja na Kanisa Katoliki nchini Brazil ambao ni wenyeji
wa Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani. Vijana wengi kutoka Barani Afrika
wameonja ukarimu wa waamini na watu wenye mapenzi mema nchini Brazil.
Vijana
wamepata fursa ya kuweza kuwashirikisha vijana wenzao: mang'amuzi ya maisha, imani,
vipaumbele na matarajio yao kwa siku za usoni. Ni matumaini ya vijana kutoka Barani
Afrika kwamba, changamoto wanazokumbana nazo, zitakuwa ni nyenzo kuu katika ujenzi
wa misingi ya haki, amani na upatanisho Barani Afrika, changamoto kutoka kwa Mababa
wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu Barani Afrika.
Makundi ya vijana kutoka
Barani Afrika yameongozwa na Maaskofu, Mapadre na Watawa wanaojihusisha na mikakati
ya shughuli za kichungaji miongoni mwa vijana. Kuna idadi kubwa ya vijana kutoka Afrika
ambao wameshiriki pia katika kazi za kujitolea na huduma kwa vijana wenzao, hali inayoonesha
umuhimu wa huduma ya mapendo kwa jamii.
Vijana wanachangamotishwa na Mama
Kanisa kuwa na matumaini ya leo na kesho iliyo bora zaidi, matumaini ambayo yanapata
chimbuko lake kutoka kwa Kristo, ambaye hadanganyi wala kudanganyika! Huu ni ujumbe
unaopaswa kufanyiwa kazi na vijana Barani Afrika katika jitihada za kuwa ni Wamissionari
miongoni mwa vijana wenzao na kwamba, wanatumwa kuwa ni wajenzi wa amani, upendo na
mshikamano katika Jamii ambamo vita, kinzani na madhulumu yanazidi kutawala na kufisha
utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.
Katika Maadhimisho
haya, vijana hawa wamejisikia kuwa kweli ni Wamissionari miongoni mwa vijana wenzao
kutoka sehemu mbali mbali za dunia na kwamba, ni uzoefu na mang'amuzi ambayo haitakuwa
rahisi sana kufutika katika akili na moyo wa mtu. Vijana waliokuwa wanahudumiwa wameonesha
moyo wa kujali na kuthamini sadaka iliyokuwa inatolewa na vijana wenzao kwa ajili
yao.
Vijana kutoka Barani Afrika wanakiri kwamba, wameguswa kwa namna ya pekee
na katekesi, liturujia na shuhuda mbali mbali zilizokuwa zinatolewa wakati wa Maadhimisho
ya Siku ya Vijana Duniani huko Rio de Janeiro. Lakini jambo ambalo linaendelea kuwagusa
watu wengi ni ukarimu wa wananchi wa Brazil. Wananchi wameonesha upendo na mshikamano
kwa mahujaji waliokuwa wanahitaji msaada wa hali na mali, lakini zaidi kwa uwepo wao.
Waswahili
wanasema "kwenye msafara wa mamba, kenge hawakosekani"! Katika Maadhimisho ya Sherehe
ya Imani kwa Vijana, hawakukosekana watu waliotaka kufanya fujo na vioja dhidi ya
Serikali na Mafundisho ya Kanisa. Baadhi yao wamekuwa wakiandamana huku wamevaa "suti
ya Adamu" kudai uhuru wa kutoa mimba dhidi ya mafundisho ya Kanisa. Lakini, hawa ni
wachache, ikilinganishwa na umati mkubwa wa vijana na watu wenye mapenzi mema waliokuwa
wanashiriki matukio mbali mbali kama sehemu ya Maadhimisho ya Juma la Vijana huko
Rio de Janeiro kwa Mwaka 2013.